Tuesday, August 16, 2016

NAIBU WAZIRI WA AFYA DK. KIGWANGALLA ALIPOFANYA UKAGUZI WA KUSHTUKIZA KITUO CHA CHESA



Naibu waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk. Hamisi  Kigwangalla, jana alifanya ziara ya kushtukiza katika kituo cha COMMUNITY HEALTH EDUCATION SERVICES AND ADVOCACY- (CHESA) kilichopo Upanga, Wilayani  Ilala, jijini Dar es salaam.

Ziara hiyo ya kushtukiza inafuatia baada ya hatua ya Naibu Waziri huyo wa Afya  Dk.Kigwangalla  kuendelea kufanya ukaguzi wa Asasi mbalimbali zisizo za kiserikali zikiwemo NGO’s na CBO zenye makosa ya kiutendaji na kimfumo  ambayo ni tofauti na taarifa zao katika usajili wa Serikalini na namna ya uendeshaji wa  wao.

Mbali na hayo kituo hicho cha CHESA kinashukiwa kuhusika na vitendo vya uhamasishaji wa mahusiano ya mapenzi ya Jinsia moja (USHOGA), ambayo ni kinyume na mila na Desturi za kitanzania pamoja na Katiba na sharia za Nchi.

“Mahusiano ya jinsia moja si kinyume na mila na desturi zetu tu. Bali hata sheria na katiba ya nchi yetu haziruhusu mfumo huo wa kimahusiano”  amesema  Dk..Kigwangalla

Aliendelea kubainisha kuwa: “Sisi kama Serikali hatujawahi kusaini mikataba yoyote ya kimataifa inayoruhusu  ushoga hivyo kwa taasisi yoyote hapa Nchini inayofanya hivyo ni kuvunja sheria za Nchi na inapaswa kuchukuliwa hatua kali za kisheria na hata kufutiwa usajili wake” aliongeza Dk. Kigwangalla.

Katika ukaguzi wa kituo hicho, Naibu Waziri wa Afya Dk. Kigwangalla  akiwa ameambatana na Kaimu Msajili wa Asasi zisizo za kiserikali kutoka Wizara anayoiongoza, Bw. Julius Mbilinyi pamoja na Mkuu wa Upelelezi  Mkoa wa Ilala, Hassan Selengu  pia wamefanya ukaguzi katika kituo hicho ili kubaini kama kuna uwepo wa vilainishi vinavyotumiwa na watu wenye mahusiano ya jinsia moja ambavyo hivi karibuni Serikali ilipiga marufuku matumizi yake hapa nchini.
 










“Serikali ilikifuta kituo cha ‘SISI KWA SISI’ kwa sababu kilihusika na tuhuma za ushawishi wa mahusiano ya jinsia moja ambacho pia wewe ulikuwa Mkurugenzi wake. Sasa tumeamua kuchunguza na kituo hichi ili tujue kama mnahusika na vitendo hivyo ili tuchukue hatua endapo itabainika ama la” ameeleza Dk. Kigwangalla.

Aidha, Naibu Waziri wa Afya Dk. Kigwangalla amemtaka Mkuu wa upepelezi  Bwana Hassan Selengu afanye uchunguzi wa kina katika kituo hicho ili kubaini pesa za misaada katika kituo hicho zinatokea wapi lakini pia ni kubaini kama kituo hicho kinajihusisha na ushawishi wa watu kujiunga na mahusiano ya jinsia moja.

“Tunawasiwasi kuwa mnapokea pesa nyingi  na misaada mingi kutoka katika Taasisi mbalimbali lakini pesa hizo zinatumika kuhamasisha mapenzi na mahusiano ya jinsia moja.

Mbali na hayo.  taarifa za usajili wa kituo hichi zinakinzana na malengo na miradi inayofanyika hapa.  Pia ipo miradi mbalimbali ambayo haijasajiliwa wala hujaitaja katika maelezo yako  lakini inafanyika katika kituo hichi” alihoji  Dk. Kigwangalla huku akimtajia baadhi ya miradi hiyo ambayo Serikali inaitambua.

Na Hashim Ibrahim (UDSM-SJMC).

No comments:

Post a Comment

POSTED TITLE

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...