Thursday, July 9, 2015

DIAMOND, ZARI KIMENUKA

OHOOO! Wakati penzi lao likitarajia matunda ya kupata kijacho miezi kadhaa ijayo, uhusiano wa Nasibu Abdul ‘Diamond na staa wa Uganda, Zarinah Hassan ‘Zari The Boss Lady’ umedaiwa kutibuka baada ya Diamond kufunguka kuwa anampenda mwigizaji wa Nigeria, Omotola Jalade Ekeinde, Amani linakupa mchapo.Mkali wa Bongo fleva Nasibu Abdul ‘Diamond.
Diamond aliitoa kauli hiyo hivi karibuni jijini Lagos alipokuwa akihojiwa redioni ambapo alipoulizwa ni wasanii gani maarufu anavutiwa nao kimapenzi, bila hiyana, mkali huyo kutoka Tandale-Dar, alisema ni Omotola, Tonto Dikeh na Genevieve Nnaji.
WAMBEA WASHIKIA BANGO
Mara baada ya Diamond kutamka kauli hiyo na kusambaa kwenye mitandao ya kijamii na baadhi ya vyombo vya habari, ‘wambea’ walilivalia njuga suala hilo na kumfikishia maneno Zari, ambaye naye anadaiwa kuyaamini na kumcharukia Diamond.

TUJIUNGE NA CHANZO
Chanzo makini kilicho karibu na Diamond kilipenyeza habari  kuwa, kauli hiyo aliyoitoa nchini Naigeria imezua mtafaruku mzito kwani Zari hakufurahishwa nayo kwa kile kichoelezwa kuwa ni kuonesha dhahiri kwamba staa huyo anayesumbua na wimbo wa Nana anaweza kuhamishia ‘majeshi’ kwa Omotola, Genivieve kama si Tonto.
“Ndugu yangu nakwambia upande wa pili kimesanuka ile mbaya baada ya Diamond kusikika akisema anawazimikia Omotola na wenzake wa Nigeria, mama la mama (Zari) huko aliko (Sauz) kafura ileile.
Nasibu Abdul ‘Diamond akiwa na Zari.
AJUTA KUMFAHAMU DIAMOND?
“Zari nakwambia anajuta kumfahamu Diamond maana anasema kwa nini awe na mwanaume ambaye anajinadi hadharani kuwapenda wanawake wengine. Pengine kama isingekuwa mimba wangeweza kuachana kabisa. Diamond ameingia kwenye kazi ya ziada ya kuhakikisha anarejesha amani haraka iwezekanavyo,” kilisema chanzo hicho.
ZARI ATAFUTWA
Jitihada za kumtafuta Zari ili aweze kuzungumzia namna ambavyo ameyapokea maneno hayo ya wambea hazikuweza kuzaa matunda kwani wapambe wake waliweka ‘ngumu’ kuvujisha namba yake japo walikiri kuwa shosti wao huyo hayuko sawa na Diamond.
“Mh! Suala la namba kama unavyojua hapa Bongo Zari hana marafiki kiivyo hivyo tukikupa namba yake tu, atajua ni sisi ndiyo tumekupa,” alisema mpambe mmoja wa Zari, Bongo ambaye hakutaka jina lake lichorwe gazetini.
DIAMOND ANASEMAJE?
Baada ya kukutana na ugumu huo, mwanahabari wetu alimvutia waya Diamond ili kuweza kumsikia anazungumziaje kuhusiana na ugomvi huo ambapo alidai si ishu kubwa, watayamaliza.
Mwigizaji wa Nigeria, Omotola Jalade Ekeinde.
“Nafikiri Kingereza kimewafanya waliovamia hilo swali na jibu langu washindwe kulielewa, maana niliulizwa kuwa, ni wanawake gani nchini Nigeria  unawakubali? Majibu yangu yaliniongoza kuwataja Omotola, Genevieve na Tonto, nikiwa kama msanii wa kiume lazima nchi yoyote nikiwa kwenye interview swali kama hili ningeulizwa tu.
“Kwa mantiki hiyo basi ningesema nisionyeshe hali ya kumkubali mwanamke yeyote Nigeria si ningeonekana ni mmbaguzi, nafikiri kuna watu wamefikisha mambo ndivyo sivyo kwa Zari na kumfanya  acharuke, ila nina imani Zari ni muelewa, yatakwisha hawezi kuyumbishwa na wambea wa kwenye mitandao,” alisema Diamond ambaye anawania Tuzo za MTV Music (Mama).Jinsi ya kumpigia kura Diamond, tembelea mtandao wa mama.mtv.com kisha fuata maelekezo.

No comments:

Post a Comment

POSTED TITLE

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...