Musa Mateja Imebainika kuwa mimba ya mwandani wa
mwanamuziki Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’, Zarinah Hassan ‘Zari The
Boss Lady’ inamwingizia jamaa huyo mamilioni ya fedha, Ijumaa limebaini
mchezo mzima.
KUMBE!
Mwandani wa mwanamuziki Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’, Zarinah Hassan ‘Zari The Boss Lady’.
Imeelezwa kwamba, katika kila shoo anayokwenda na mama kijacho huyo
amekuwa akilamba dau kubwa kwani wengi wanahudhuria burudani inayotolewa
na Diamond ili kumuona Zari akiwa na kibendi.Uchunguzi wetu ulibaini
kwamba, ujauzito wa Zari kwa sasa unamuingizia mkwanja mrefu Diamond
kufuatia kila shoo anayohitaji kwenda kufanya, mapromota wengi wamekuwa
wakimtaka aende na Zari ili tu mashabiki wamshuhudie.
TUJIUNGE NA CHANZO
Katika uchunguzi wake, Ijumaa lilizungumza na
vyanzo mbalimbali akiwemo mtu wa ndani ya Wasafi Classic Baby (WCB)
ambaye alithibitisha kuwa ni kweli uwepo wa mimba ya Zari kwa sasa
umeongeza mamilioni ya fedha kwa Diamond kupitia shoo ambazo amekuwa
akihitajika na mapromota kwenda na Zari.
DIAMOND ASHTUKIA
Chanzo hicho kilimwaga ‘ubuyu’ kuwa, Diamond
ameshalishtukia jambo hilo kiasi kwamba kuna sehemu sasa analazimika
kwenda na Zari kwa siri.
Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz akibusu mimba ya Zari.
ZARI AFICHWA MWANZA
Ilifahamika kwamba, kwenye Shoo ya Jembeka
iliyofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita jijini Mwanza, Diamond
alikwenda na Zari kwa kificho kikubwa kiasi kwamba hata umati
uliyojitokeza kumpokea uwanja wa ndege jijini humo hawakuweza kumuona
kwa kuwa makubaliano yake na waandaaji hayakumhusu Zari.
“Alichokifanya Diamond ni kumficha hotelini kwa kuwa katika shoo hiyo
mapromota walikuwa hawakuelewana naye kwenda na Zari kama ilivyo kwenye
shoo nyingine anazofanya kwa sasa,” kilisema chanzo hicho cha kuaminika
na kuongeza:
“Ni kitu ambacho Watanzania wengi hawakijui lakini ukweli uko hivyo
kwamba, Diamond kwa sasa anavunja mkwanja mara mbili anapokuwa na Zari.”
BEI MARA MBILI?
Ilidaiwa kwamba kama Diamond alikuwa anachukua
Sh. milioni 25 kwa shoo za ndani, kwa sasa akiwa na Zari ni mara mbili
yake kwa hiyo inakuwa si chini ya Sh. milioni 50.
SHOO ZA KUMWAGA ZA NJE
Chanzo hicho kilieleza kwamba kwa shoo za
nje ndiyo usiseme na tayari ameshaingia mikataba ya fedha ndefu kwenye
nchi mbalimbali akiwa na Zari zikiwemo, Afrika Kusini ‘Sauzi’, Nigeria,
Ghana, Cameroon, Togo, Angola na nyingine kibao.

DIAMOND ABANWA, AFUNGUKA
Baada ya kunyetishiwa ubuyu huo, mwanahabari wetu alimtafuta Diamond na
kumbana ili afunguke juu ya hilo ambapo alipopatikana alikiri kwamba ni
kweli kwa sasa mapromota wengi wamekuwa wakimhitaji kwenye shoo akiwa
na Zari.
Diamond alisema kuwa, jambo hilo ni zuri ila kila mmoja ana
malipo yake kwa maana wakitaka aende naye bei inakuwa tofauti
ukilinganisha anapokwenda mwenyewe au na timu yake ya Wasafi.
Diamond: Nikiwa naenda kwenye events (matukio) namuuliza kwanza
promota kama atahitaji niende na Zari? Akinijibu ndiyo, gharama
inaongezeka.Ijumaa: Kwa hiyo unamaanisha kwa sasa ukienda kwenye shoo
bila Zari kuna bei yake na ukienda naye unatakiwa ulipwe bei tofauti?
Diamond: Naam, namaanisha kwamba nikienda na Zari, lazima kuwepo na gharama za uwepo wake.
Ijumaa: Ni jambo gani lililokufanya kushtukia hilo hadi unasema hivyo?
Diamond: Ujue sasa hivi imefikia hatua nikiposti kwenye peji yangu
kwamba kuna shoo nitaenda na Zari, idadi ya watu inaongezeka hata kama
sitaingia naye ukumbini.
Ijumaa: Zari anajisikiaje mimba yake kufanywa ya maonesho?
Diamond: Zari ni mtu wa hekaheka hivyo hana tatizo kwani usalama wake upo wa kutosha.