Thursday, January 16, 2014

HIVI NDIVYO WEMA SEPETU ALIVYOFIRISIWA KILA KITU NA BWANA AKE WA ZAMANI


Wema Isaac Sepetu.
Na Imelda Mtema
ZILE tambo, mbwembwe na majigambo ya Miss Tanzania 2006/07, aliye pia msanii wa filamu Bongo, Wema Isaac Sepetu, zimefika mwisho kufuatia kunyang’anywa samani za ofisi yake ya Endless Fame Film Production na aliyekuwa mpenzi wake, Clement ‘kigogo wa ikulu’ na sasa amebaki mweupe, Amani limepakuliwa ikiwa imeiva.
Kwa mujibu wa chanzo chetu, tukio hilo la aibu lilijiri hivi karibuni kwenye ofisi hiyo ya Wema iliyopo Mwananyamala-Komakoma jijini Dar.
KIGOGO WA IKULU AVAMIA NA MABAUNSA
Habari za uhakika zinadai kuwa, siku ya tukio, Clement akiwa ameongozana na watu waliosadikiwa kuwa ni mabaunsa, walivamia ofisi hiyo aliyomfungulia mlimbwende huyo na kukomba vitu vyote vya thamani alivyomnunulia wakati wa mapenzi motomoto (hakuna lenye mwanzo lisilo na ncha).
KUMBE ALIKODI CANTER
Kama njiwa apelekaye ujumbe muhimu wa huba, mtoa taarifa huyo alizidi kumwaga ‘upupu’ kuwa, siku hiyo Clement mbali na gari lake la kifahari, pia alitinga akiwa na gari aina ya Canter ambapo bila maswali wala maelezo achilia mbali ufafanuzi, alikusanya vifaa vyote na kuvirundika kwenye gari.
Wema akiwa katika ofisi yake kabla ya kunyang'anywa samani zilizomo.
IDADI YA VITU VILIVYOBEBWA

Vifaa hivyo ni tarakishi (computer), kamera ya kurekodi sinema (video camera), vifaa vya kurekebisha hali ya hewa (air conditioner), vifaa vya kuhifadhia umeme wa ziada, uninterruptible power supply (ups) pamoja na vifaa vingine zikiwemo nyaya za umeme na kuiacha ofisi nyeupe kama uwanja wa mpira.

“Hali ni mbaya sana, jamaa (Clement) alichukua kila kitu ndani ya ofisi hiyo kuanzia kompyuta, kamera hata nyaya! Hivi tunavyoongea, ofisi haina kitu kabisa,” kilisema ‘kikulacho’ hicho.

CHANZO NI DIAMOND
Mpashaji huyo alizidi kuyapa utulivu masikio ya mwandishi wetu kuwa, chanzo cha kigogo huyo kufanya ‘umafia’ huo ni kitendo cha Wema kurejesha penzi lake kwa ‘mtemea maiki’ wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul Jumaa ‘Diamond Platnumz’.
Ofisi ya Wema kwa ndani.

Taarifa hizo zilieleza kuwa, kitendo hicho kilichochea hasira za Clement, hasa pale Diamond alipohojiwa kuhusu kuingilia penzi hilo na kujibu hamwogopi mtu, “ndiyo maana Clement akaamua kumwaga ugali baada ya wawili hao (Wema na Diamond) kumwaga mboga,” kiliongeza chanzo.
HEBU MSIKILIZE WEMA

Ili kujua yapi ni maziwa na lipi ni tui juu ‘niuz’ hizo, mwandishi wetu alimtafuta Wema na kukutana naye laivu juzi ambapo alikiri kukumbwa na zahama hiyo huku akionesha mshangao wa wazi kwa kitendo alichofanyiwa na ‘zilipendwa’ wake huyo.
 
Geti la kuingia katika ofisi hiyo.

“Ni kweli kabisa Clement amefanya hivyo, lakini nashangaa na ni mara yangu ya kwanza kuona wapenzi wakiachana mwanaume anaamua kuchukua vitu vyote alivyowahi kumnunulia au kumpa.
“Huo ni ushamba na unyanyasaji, akumbuke kwamba alipokuwa na mimi alinitumia pia,” alisema Wema na kuongeza:
“Hata hivyo, namshukuru Mungu, vitu vyote alivyochukuwa Clement, baby (Diamond) kasema ataninunulia, wiki mbili hazitapita.”
Wema alikwenda mblele zaidi kwa kuonesha machungu yake kwa kigogo huyo pale aliposema: “Kwanza nasikia vitu vyenyewe alipofika nyumbani kavimwaga nje maana ndani hakuna nafasi.”
KAANZA MWAKA VIBAYA

Mwanzoni mwa mwaka huu, Wema alikumbwa na mkasa wa kunyang’anywa lile gari la kifahari alilodai ni lake, Audi Q7 baada ya kusemekana kuwa halikuwa lake.
Kumbe gari hilo alipewa na Clement ambaye naye alilikopa kwa thamani ya shilingi milioni 90 kutoka kwa mtu aliyejulikana kwa jina la Shadrack Tweve.
Tweve, baada ya kuzungushwa sana kulipwa fedha hizo, alikimbilia Mahakama ya Wilaya ya Ilala ambapo hakimu aliamuru gari hilo likamatwe na kurejeshewa mlalalamikaji huyo.
 PENZI LA WEMA, KIGOGO WA IKULU
Uhakika ni kwamba, penzi kati ya Wema na kigogo huyo halipo tena na kwa sasa jamaa ana demu mwingine (jina tunalo) ambapo mapaparazi wetu wanaendelea kufuatilia kwa karibu ili kuwanasa katika mazingira yoyote yale

No comments:

Post a Comment

POSTED TITLE

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...