Thursday, May 28, 2015

KAJALA AMWANGUKIA WEMA

KWELI dhamira inauma! Staa mkali wa sinema za Bongo, Kajala Masanja ameamua kukifungua kinywa chake na kusema kuwa anamwomba msamaha zilipendwa wake katika urafiki, Wema Isaac Sepetu kwa mabaya yote aliyomtendea, Amani linakupa zaidi.
Staa mkali wa sinema za Bongo, Wema Sepetu.
Akizungumza katika mahojiano maalum na  mapaparazi wetu mapema wiki hii jijini Dar, Kajala alisema hata kama kuna chuki ya ukubwa kwa kiasi gani baina yao lakini Wema atabaki kuwa mtu muhimu sana katika maisha yake mpaka atakapoaga dunia!
“Najua mimi na Wema hatuko sawasawa. Lakini namwomba anisamehe sana. Naumia kila siku. Yeye ni mtu muhimu sana katika maisha yangu. Atambue hilo,” alisema Kajala.

ATAJA UMUHIMU
WA WEMA
Akizungumzia umuhimu wa Wema kwake, Kajala alisema:
“Kwanza iweleweke kwamba, namchukulia ni mtu muhimu kwa vile hakukuwa na mwingine wa kunitolea zile shilingi milioni 13 kule mahakamani (Kisutu).“Bila Wema  mimi leo hii ningekuwa natumikia kifungo cha  miaka 7 jela, lakini kutokana na huruma yake alinisaidia hivyo ataendelea kuwa mtu muhimu sana kwangu.”

TATTOO YAKOLEZA
Staa huyo alikwenda mbele zaidi kwa kusema kuwa, baada ya kunusurika na kifungo kwa Wema kumlipia fedha hizo alijichora tattoo yenye jina la Wema eneo la mgongoni juu, akasema:
“Tattoo ya jina la Wema,  niliyojichora inadhihirisha wazi haiwezi kufutika daima na daima na hiyo inaonesha kuwa ni jinsi gani Wema yupo ndani ya moyo wangu.”

Staa mkali wa sinema za Bongo, Kajala Masanja.
ATAMANI WAENDE NJE YA DAR
Kajala aliongeza kuwa kuna wakati anatamani yeye na hasimu wake huyo waende mbali kabisa na Jiji la Dar, hata visiwani ambapo hakuna watu wanaowazunguka ili wakazungumzie tofauti zao na kila mmoja akaeleza makosa yake kwa mwenzake na wakawekana sawa.

Staa huyo aliongeza kuwa kipindi cha sasa ni cha wanawake kushirikiana na kuleta maendeleo na siyo kuyajenga  mabifu siku hadi siku kitu ambacho si sahihi kabisa na hawawezi kuendelea hata siku  moja.
“Ninachojua mimi mabifu hayaleti maendeleo hata siku moja, badala yake yanarudisha nyuma kitu ambacho siyo kizuri, hasa kwa sisi wanawake tunaotakiwa tujitume siku hadi siku ili kujikwamua na maisha magumu. “Kikubwa ni kusameheana ili tuweze kukutana na kufanya kazi kwa bidii tulete mabadiliko katika tasnia yetu ya Bongo Movies,” alisema Kajala.
KAJALA AKITANGULIA KUAGA DUNIA
Kajala: “Na ili kuonesha kuwa niko tayari kwa amani na Wema, siku ikitokea mimi nikaaga dunia basi rafiki yangu kipenzi Wema asiache kuja makaburini kunizika.”

WEMA ASAKWA ASEME NENO
Juzi saa nne asubuhi, Amani lilimtafuta Wema kwa njia ya simu ili azungumzie kauli ya Kajala lakini hakupatikana mara moja hewani hata pale alipofuatwa nyumbani kwake, Makumbusho-Kijitonyama, hakupatikana baada ya watu wake wa karibu kusema alikuwa bado amelala.

Hata hivyo, katika mahojiano kwenye kipindi cha redio moja ya jijini Dar hivi karibuni, Wema aliulizwa swali kuhusu uhusiano wake na Kajala ambapo alisema aliwahi kumfuata siku za nyuma baada ya kumkosea na kumwambia ‘laivu’ lakini yeye (Kajala) akaenda kuyasema kwingine tena vitu vingine kabisa na si vile alivyomwambia.“Kuhusu kupatana nasikia kuwa ameposti kwenye mitandao anataka tupatane. Mimi milango iko wazi,” alisema Wema.

Mama Kajala.
CHANZO CHETU
Chanzo chetu kimoja kilizungumza na Amani na kusema: “Tatizo la Kajala ni staili anayoitumia kuomba msamaha. Si vizuri aseme kwenye mitandao yeye anatakiwa kutafuta wakubwa ambao watawaweka chini na kuzungumza nao. Tena basi Timu Kajala na Timu Wema wamebariki wapatane. Na wazazi wao wameombwa wasiwaingilie kwenye uamuzi wao.”

No comments:

Post a Comment

POSTED TITLE

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...