Monday, May 18, 2015

LISSU: MARUFUKU WANANCHI KUNYANYASWA KISA MICHANGO

Singida Mashariki ni moja kati ya majimbo ya uchaguzi yaliyopo Wilaya ya Singida Vijijini mkoani Singida, likiongozwa na Mheshimiwa Tundu Antipas Lissu kwa tiketi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema). Awali, jimbo hilo lilikuwa likijulikana kama Singida Kusini kabla ya kugawanywa mwaka 2010 na kupata majimbo mawili, Singida Mashariki na Singida Magharibi.
Mheshimiwa Tundu Antipas Lissu kwa tiketi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).
Kama ilivyo kawaida, gazeti hili lilifanya ziara kwenye jimbo hilo na kuzungumza na wananchi walioeleza kero zinazowasumbua na jinsi mbunge wao alivyotimiza ahadi alizowaahidi alipogombea mwaka 2010.
MATATIZO YA WANANCHI
Katika ziara yake jimboni humo, Uwazi lilibaini matatizo yanayowakabili wananchi wa Singida Mashariki yakiwemo kunyanyaswa wakilazimishwa kulipa michango ya ujenzi wa maabara kwenye shule, ukosefu wa mawasiliano ya simu kwenye baadhi ya maeneo, uchakavu wa vyumba vya madarasa, uhaba wa walimu, ukosefu wa vifaa vya kufundishia kwa shule nyingi za jimbo hilo pamoja na vijiji vingi kutokuwa na nishati ya umeme.

SEKTA YA MAWASILIANO
Wananchi waliozungumza na Uwazi, walisema suala la mawasiliano limekuwa tatizo sugu kwani sehemu nyingi hakuna minara ya makampuni ya simu za mikononi, hali inayosababisha wananchi kukosa mawasiliano au sehemu nyingine kulazimika kupanda milimani au kwenye miti kutafuta mawasiliano mazuri.


“Yaani ukitaka kupiga simu lazima uangalie sehemu yenye miinuko au upande kwenye mti ndipo uweze kuwasiliana vizuri, afadhali kipindi hiki tangu Lissu aingie madarakani tunaona tofauti kwani kampuni za simu zimeanza kujenga minara kuliko ilivyokuwa mwanzo, hali ilikuwa mbaya, tunaomba aendelee kutupigania tupate mawasiliano mpaka vijijini,” alisema Suzana Lyantulu, mkazi wa Kijiji cha Makyungi.
SEKTA YA ELIMU
Uwazi lilibaini kwamba, katika jimbo hilo kuna matatizo mengi katika sekta ya elimu lakini kubwa, ni suala la wananchi kulazimishwa kuchangia elimu na wakati mwingine kujikuta wakipokonywa mifugo yao au kulipishwa faini kubwa, jambo ambalo Mheshimiwa Lissu amekuwa mstari wa mbele kulizuia.

“Tunamshukuru Mheshimiwa Lissu, tulikuwa tunanyanyasika sana kipindi cha nyuma, tunalazimishwa kuchangia elimu kwa nguvu wakati fedha tunazotoa zinaishia kwenye mifuko ya wajanja wachache.
“Mbunge wetu akaingilia kati na kutukataza kuchangia pesa zozote mpaka tuambiwe kwanza tulizochanga awali zimefanya kazi gani. Kwa kweli Lissu ni mpiganaji na ametimiza ahadi yake ya kukomesha michango kama alivyoahidi wakati akiomba kura,” alisema Nicodemus Kachenje mkazi wa jimbo hilo.
 
SEKTA YA AFYA
Wakigusia kero za afya, wakazi wa jimbo hilo walisema viongozi wengi wa serikali wanaendekeza ufisadi kiasi cha kusababisha majengo ya zahanati kama Kimbwi, ujenzi wake kusimama baada ya fedha zilizochangwa na wananchi kutafunwa na wajanja.

“Tunashukuru mbunge wetu ameingilia kati na kusema tusichange tena fedha zozote mpaka zile tulizochanga tuambiwe kwa uwazi zimefanya kazi gani, viongozi wengi ni mafisadi huku kwetu,” alisema Cleopa Zakaria.
Kero zingine ni ubovu wa miundombinu zikiwemo barabara nyingi za jimboni humo ambazo hazina ubora unaohitajika na ukosefu wa umeme katika baadhi ya vijiji.

MAELEZO YA MBUNGE
Baada ya kusikiliza maelezo ya wananchi, Uwazi lilimtafuta mbunge wa jimbo hilo, Mhe. Lissu ambaye alisema anazitambua vyema changamoto za wananchi wake na kueleza jinsi alivyojitahidi kuzitatua.“Nilipoingia madarakani, mambo mengi yalikuwa hovyo sana jimboni kwangu, ufisadi, rushwa na unyanyasaji wa wananchi kwa sababu ya michango ulikuwa mkubwa lakini nimejitahidi kadiri ya uwezo wangu kuwasaidia.

“Suala la wananchi kulazimishwa kuchangia fedha kwa ajili ya shughuli za maendeleo halikubaliki kwa sababu hilo ni jukumu la serikali na kila mwaka bajeti kubwa zinatengwa kwa ajili ya kazi hiyo.
“Wanaokataa kuchanga fedha ni wanaoniunga mkono kwani wakati nawaomba kura niliahidi kuwafutia michango yote wanayochangishwa na serikali ambayo inaliwa na watendaji wa serikali za mitaa, hatuwezi kuchanga fedha wakati serikali ina uwezo wa kujenga maabara na zahanati kama ilivyoahidi,” alisema Lissu na kuongeza kuwa anawaomba wananchi wake waendelee kumuunga mkono ili akamilishe mambo yote aliyowaahidi ikiwa ni pamoja na kuwakomboa kutoka kwenye lindi la umaskini.

No comments:

Post a Comment

POSTED TITLE

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...