Thursday, April 9, 2015

MGOMO WA MADEREVA WA VYOMBO MBALIMBALI VYA MOTO WAANZA LEO

Muonekano wa abiria wakiwa stendi ya Ubungo jijini Dar es Salaam (Picha na Maktaba).
MADEREVA wa vyombo mbalimbali vya moto, nchi nzima leo asubuhi wamegoma kusafirisha abiria ili kuishinikiza serikali kuondoa kero mbalimbali zinazowakabili ikiwemo ukosefu wa ajira za uhakika pamoja na agizo la kutaka kwenda kusoma.
Awali kabla ya mgomo wa leo, Katibu wa Muungano wa vyama vya madereva Bw. Rashid Saleh, alisema baadhi ya kero zitakazopelekea mgomo wa leo ni pamoja na suala la kurudia kusoma kila wanapohuisha leseni zao ambayo wanadai ni aina nyingine ya unyanyasaji kwa maelfu ya madereva nchini, ambao kwa kipindi kirefu wamekuwa hawana mfumo mzuri wa ajira licha ya kutupiwa lawama kibao kuwa wao ndio chanzo cha ongezeko la ajali.
Katibu huyo wa Muungano wa Vyama vya Madereva alitaja kero nyingine kuwa ni hatua ya Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) kutamka hadharani kuwa vyeti walivyonavyo madereva hao sio halali na walipanga leo kukutana na Waziri wa Kazi na Ajira kwa ajili ya kuzungumzia kero hizo kwa lengo la kuepusha kutokea kwa mgomo huu.
Saleh aliwataja madereva wanaounda muungano huo kuwa ni wa bodaboda, bajaj, teksi, daladala, mabasi ya safari fupi, mabasi ya safari ndefu na za nje ya nchi pamoja na madereva wa magari yote ya mizigo.
Kwa mujibu wa kiongozi huyo wa muungano wa madereva, wamegoma maana wamechoka kudharauliwa hata kwa mambo ya msingi yanayogusa maisha yao.
Baadhi ya dharau alizozitaja ni pamoja na wamiliki wa mabasi (yaani waajiri wao) kuwaita wao ni wahuni ilhali ni watu wazima, wenye familia, wanaofanya kazi halali na wanaohitaji kuheshimiwa.

No comments:

Post a Comment

POSTED TITLE

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...