UKITAKA kuwaudhi Watanzania wengi – wasomi na
wajinga, wafupi na warefu, walevi na wasiotumia vileo – unachotakiwa
kufanya ni kutaja makosa aliyoyafanya Rais wa Kwanza wa Tanzania, Julius
Kambarage Nyerere akiwa madarakani.
Tundu Lissu, Mbunge wa Singida Mashariki, katika mijadala ya kuweka
mambo sawa kitaifa, aliposema: “Nyerere hakuwa Mungu” akimaanisha
yaliyofanywa na kusemwa na Nyerere hayakuwa msahafu, alisakamwa na watu
kibao kwa kusema ukweli wa wazi hata kwa mtoto mdogo!
Wanaoisoma safu hii wakiwa wamenuna wafahamu kwamba Nyerere alikuwa
kiongozi wa nchi hii hivyo historia aliyoiacha itasemwa na Watanzania
kwa miaka nenda-rudi.
Nyerere atazungumziwa sana kwa vile alituachia urithi wa mambo mengi
yakiwemo ambayo leo yanaendelea kutukosesha furaha ya kweli kisiasa na
kiuchumi na ambayo warithi wake wanayatumia kupitia jina lake.
Katiba
ya sasa ya mwaka 1977 iliyotungwa wakati wa utawala wake, ambayo wengi
wanaiita ‘Katiba ya Nyerere’, ndiyo chimbuko la matatizo mengi ya
kisiasa yanayoendelea kuleta giza na kuwakosesha Watanzania wengi
tabasamu la kitaifa.
Katiba hiyo iliandikwa na watu wachache na kupitishwa na watu
wachache kwa kivuli cha bunge, wakati huo likiwa na wabunge wa Chama Cha
Mapinduzi (CCM) tu! Heshima na woga wa Watanzania kwa kiongozi wao
huyo viliwafanya ‘wakubali yaishe’ na katiba hiyo ikaanza kutumika hadi
leo!
Kabla ya katiba hiyo ya 1977, kulikuwa na katiba zenye sura hiyohiyo
ya kukidhi utawala wa serikali yake ya chama kimoja – baada ya kuvipiga
marufuku vyama vingine vya siasa mwaka 1965! Nyerere kama binadamu na
wanasiasa wengine alikuwa hakosi maajabu!
Alikuwa anakiri kwamba katiba aliyokuwa anaitumia ilikuwa ya
kidikiteta, na kwamba ilikuwa inatoa mwanya kwa mtu yeyote kuitumia na
kuendesha nchi kidikteta. Ajabu ni kwamba aliendelea kuitumia katiba
hiyohiyo mpaka anaondoka madarakani mwaka 1985! Kwa wasiokumbuka,
Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliitawala Tanzania kwa miaka ipatayo
25!
Kwa Nyerere kukiri kutumia katiba ya kidikteta, watu waliokuwa
wanampenda na kumwogopa, walitegemea katiba hiyo ingekoma baada ya yeye
kuachia madaraka na hivyo kutoa mwanya wa kuandikwa katiba mpya
isiyokuwa ya kuogopana wala kutishana.
Lakini haikuwa hivyo! Aliondoka na kuiacha ikaendelea kutumiwa na
‘waliopokea kijiti’ kutoka kwake ambapo maudhui yake yameingizwa katika
Katiba Inayopendekezwa.Kama enzi ya Nyerere, Katiba Inayopendekezwa
inampa rais madaraka ya kifalme ya kuteua viongozi wote muhimu wa
kitaifa kuanzia wilayani na mikoani, mawaziri, makatibu wakuu wa wizara,
wakuu wa majeshi ya ulinzi na polisi, usalama wa taifa, wakuu wa
mashirika na taasisi za umma na kadhalika.
Miongoni mwa taasisi nyingi anazoteua viongozi wake ni pamoja na Tume
ya Taifa ya Uchaguzi! Hilo ndilo chimbuko kubwa la mikanganyiko yote
ya maisha ya kisiasa katika dhamira ya kujenga demokrasia ya kweli ya
umma.
Tume ya Taifa ya Uchaguzi inaendelea kuwa chini ya ‘ajira’ ya rais
ambapo wajumbe wake wanajua rais ndiye mwenye uwezo wa kuwafukuza
kazi.Kwa kifupi, katika mfumo huu, watumishi wote wa taasisi za umma,
wanaoteuliwa na rais wataendelea kuwajibika kwa rais ambaye kimsingi
ndiye mwajiri wao -- si wananchi!
Kumlimbikizia madaraka rais ni
kuendelea kuyaweka maisha ya wananchi chini ya ghilba na utashi wa
wanasiasa badala ya kuwapa wananchi uwezo wa kuchagua wakuu wa wilaya na
mikoa sehemu zao.
Mfano wa ghilba za wanasiasa kuhusu ‘Katiba ya Nyerere’ ni kuhusu mgombea binafsi.
Katiba hiyo ya 1977 ilikuwa na kifungu kilichoruhusu wagombea binafsi
wa nafasi zote za kisiasa, bila kulazimika kuwa katika chama chochote.
Kifungu hicho kilikuwepo ‘kimyakimya’ bila kutumiwa, na bila wananchi
kuambiwa kwamba kipo.
Baada ya mfumo wa vyama vingi kuanza, kiongozi wa Democratic Party,
DP, Christopher Mtikila, alieleza nia ya kutumika kwa kifungu hicho,
jambo lililopingwa bila sababu za msingi na wanasiasa waliokuwa
madarakani hadi likafika mahakamani.
Kwa vile lilikuwemo katika katiba, mahakama bila kusita ilikubaliana
naye. Lakini katika maajabu ambayo yamekuwa yakifanywa na wanasiasa wa
nchi hii, bunge la CCM lilifanya mabadiliko ya dharura, mabadiliko ya
11 ya Katiba katika Ibara ya 34 na kukifuta kifungu hicho kilichoruhusu
wagombea binafsi!
Tendo hilo lilifanyika Nyerere akiwepo, na hakusema lolote, licha ya
kuwa alikuwa amesisitiza kifungu hicho kitumike katika siasa za vyama
vingi alipohutubia mkutano wa Siku ya Wafanyakazi mjini Mbeya!
Katiba Inayopendekezwa imeridhia wagombea binafsi lakini kwa masharti magumu ajabu! Kwa nini? Hizo ndizo ghilba za wanasiasa.
Miaka 35 tayari imepita tangu ‘Katiba ya Nyerere’ ilipoanza kutumika
katika juhudi za kuimarisha utawala wa chama kimoja ambapo nguvu na
hatamu zote za kuongoza maisha ya watu zilikuwa mikononi mwa mtu mmoja.
Kuendelezwa
kwa ‘maudhui’ ya Katiba ya 1977 – leo mwaka 2015 – kwa ghilba za
kupitia Katiba Inayopendekezwa, ni kufungua mlango ambao wanaosimamia
ghilba hizo watakuja kuleta majanga kwao na kwa wananchi wenzao na
kuishia kujuta!
Kuwarudisha Watanzania katika siasa za miaka 35 iliyopita ni kuwaonea na ni dhambi.
Umefika
wakati kwa viongozi kuwaogopa wananchi ambao ndiyo waajiri wao na si
wananchi kuwaogopa viongozi! Hapo ndipo tutakapojenga jamii ya
kutolipiziana visasi katika kupeana ‘vijiti’ vya kisiasa. Wahenga
walisema: Majuto ni Mjukuu!
No comments:
Post a Comment