WAKATI hofu ya ugaidi wa Kundi la Al Shabaab la Somalia ikiwa bado
imetanda kufuatia mauaji ya wanafunzi 146 wa Chuo Kikuu cha Garissa
nchini Kenya, hisia za kuwepo kwa bomu imewakumba watu mbalimbali pamoja
na wasomi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, baada ya kitu kilichodhaniwa
kuwa bomu kukutwa katika kituo cha mabasi ya daladala kijulikanacho
kama Kontena, kilichomo eneo la chuo hicho.
Tukio hilo lilitokea mchana wa Aprili 14, mwaka huu ambapo wanafunzi
hao walionekana kuushangaa mfuko mweusi uliokuwa pembeni ya kituo hicho,
ambao ndani yake kulionekana kiboksi cheusi, kilichowafanya kuamini
kuwa ni bomu.
Waandishi wetu waliokuwa wakipita eneo hilo, waliwataarifu walinzi wa
chuo hicho, ambapo mmoja wao alienda kushuhudia mfuko huo. Kabla ya
kuufikia, aliwatawanya wanafunzi waliokuwa wametaharuki na kuusogelea,
lakini hofu ya mlipuko ilimfanya asiuguse, badala yake akaenda kutoa
taarifa kituo cha polisi chuoni hapo kwa ajili ya msaada zaidi.
Katika kituo cha Polisi Chuo Kikuu, askari aliyejitambulisha kwa jina
la Sajenti Buwa, aliambatana na mlinzi huyo hadi eneo la tukio na kwa
ujasiri wa aina yake, polisi huyo aliufungua kwa tahadhari mfuko huo na
kubaini kuwa halikuwa bomu, bali ni betri ya pikipiki iliyozungushiwa
nyaya.“Hii ni betri ya pikipiki, hapa hamna kitu, hili siyo bomu lakini
hili siyo la kupuuza, aliyeweka alidhamiria kitu...,” alisema Sajenti
huyo.
Waziri wa Mambo ya Nje, Habari na Mawasiliano wa Umoja wa Wanafunzi
wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (DARUSO), Joseph Nyalomba, alikiri
kupata taarifa za kuwepo kwa kitu kilichosadikiwa kuwa ni bomu.
“Tulisikia uvumi huo, lakini niliwasiliana na watu wa usalama wakasema
kuwa ilikuwa ni betri ya pikipiki iliyotelekezwa na mtu asiyejulikana.
Nawatoa hofu wanafunzi kuwa, ulinzi wa chuoni tumejitahidi
kuuimarisha hivyo wasiwe na hofu, zaidi nawataka wawe walinzi wao kwa
wao na kuripoti mara moja kwa watu wa usalama wakiona jambo tofauti,”
alisema waziri huyo.
Imeandaliwa na Chande Abdallah, Issa Mnally, Shani Ramadhani, Mayasa Mariwata na Deogratius Mongela
No comments:
Post a Comment