Sunday, March 1, 2015

SIMBA YASHUSHA WATAALAM KUTOKA UHOLANZI

Rais wa Simba, Evans Aveva aksisitiza jambo.





Uongozi wa Simba umetangaza rasmi kuwa tayari wamepata kampuni kutoka Uholanzi ambayo ndiyo itajenga uwanja wao wa Bunju, ulioshindikana miaka nenda rudi.
Akizungumza kwenye mkutano mkuu wa klabu hiyo, uliofanyika leo kwenye  Bwalo la Polisi, Oysterbay

Rais wa Simba, Evans Aveva
aliwatoa dukuduku wanachama wa klabu yao kuhusu maendeleo ya uwanja huo kwa kusema kuwa kuna makapuni mawili, jingine kutoka hapa nchini.
Ni mimi... Wanachama wakitaka kuchangia katika mkutano. Kulia aliyenyoosha mkono ni Mwenyekiti wa Matawi Dar, Ramadhan 'Dong King'.
Makamu Rais, Geoffrey Nyange Kaburu.

Aidha Aveva alisema ujenzi wa uwanja huo unatarajiwa kuanza hivi karibuni, baada ya kukamilisha kila kitu, ikiwemo pamoja na kuandaa michoro ya kiwanja hicho.
“Kimya chetu, wengi wanaweza kudhani tumeupotezea uwanja wetu, hapana, tupo katika mikakati ya kuendeleza ujenzi baada ya kukamilisha michoro ya kiwanja. Tumepanga kuanza na hosteli kwa ajili ya wachezaji pamoja na viwanja viwili vya mazoezi.
“Ujenzi utaanza hivi karibuni na tunaamini utakuwa tayari kufikia msimu ujao na maandalizi yote ya kujiandaa na msimu ujao, ndio utatumika,” alisema Aveva.
Katika mkutano huo, wanachama walijitokeza kwa uchache sana, ambapo takwimu za awali walihudhuria watu 380, huku idadi kamili ya wanachama timu hiyo ikijulikana kuwa ni zaidi ya 10,000.

Mwenendo mbaya wa timu
Katika mkutano huo, wanachama walitaka kupata majibu ya kina kuhusu mwenendo mbaya wa timu, ambapo Aveva alifunguka sababu kuu tatu zinazoifanya timu yao kuyumba.

“Timu yetu ina changamoto kadhaa kwa sasa na hilo tukubaliane. Kwanza kikosi chetu ni kichanga, kwa maana kwamba kinaudwa na wachezaji wengi ambao hawana uzoefu, ni suala la kumpa muda mwalimu (Goran Kopunovic). Pili, timu kwa sasa haina hela. Angalia vyanzo vya mapato ya timu kwa mwezi ni milioni 300, lakini mahitaji ya mwezi ni zaidi ya milioni 49 kwa ajili ya malipo ya mishahara ya wachezaji na wafanyakazi.” 

Mgawanyiko ndani ya klabu
Aidha Aveva akafunguka juu ya taarifa zilizozagaa kwa sasa kuwa timu hiyo inafanya vibaya kutokana na kutokuwepo kwa maelewano ndani ya kamati za juu, pamoja na sakata la Simba Ukawa.

“Hakuna magwanyiko kama wengi wanavyosema, ni maneno tu ya watu. Mimi na ndugu yangu Kaburu (Geoffrey Nyange) tunaelewana na tunashirikiana tangu enzi na enzi na si kama wanavyosema. Kuhusu wanachama tuliowafukuza, kuna maneno mengi yaliongelewa baada ya kuwaondoa (wanachama 71, walifukuzwa kwa kosa la kufungua kesi katika mahakama za kiraia), kama wanataka yaishe, basi wafuate taratibu ikiwemo pamoja na kufuta kesi mahakamani. Binafsi siamini kama matokeo mabaya chanzo ni wao kama wanaihujumu timu.” 



No comments:

Post a Comment

POSTED TITLE

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...