Sunday, March 15, 2015

RAY C: MAMA YANGU ANAUMWA SANA

Musa Mateja STAA wa Bongo Fleva, Rehema Chalamila ‘Ray C’, ambaye anatumia dozi ya kumwezesha kuacha matumizi ya madawa ya kulevya, amesema kuwa mama yake mzazi yu mgonjwa sana, akisumbuliwa na maumivu makali, Ijumaa Wikienda lina mkasa kamili.
Mama mzazi wa Ray C, Margaret Mtweve.
Akizungumza na gazeti hili mwishoni mwa wiki iliyopita, staa huyo alisema kwa zaidi ya siku tatu mfululizo, mama yake alishindwa kupata usingizi kutokana na maumivu ya mifupa ya miguu yaliyomfanya avimbe miguu, kitendo kilichosababisha ajikute akilia kama mtoto mdogo.

Rehema Chalamila 'Ray C'.
“Ujue mara ya kwanza aliuguaga na kulazwa Hospitali ya Taifa Muhimbili, baadaye Mungu alimjalia akapona lakini naona ugonjwa wake umerudi tena. Anasumbuliwa na mifupa ambayo inamfanya wakati mwingine avimbe miguu hadi anashindwa kutembea,” alisema nyota huyo maarufu kama Kiuno Bila Mfupa.
Alisema mama yake amekuwa akipata shida kutembea kiasi kwamba Ijumaa iliyopita, alimpeleka hospitali ya Wachina iliyopo Sinza ili kupata vipimo na dawa, lakini haikusaidia.
“Hapa ninapoongea na wewe leo Jumamosi Machi 14, nipo kwenye Hospitali ya Misheni hapa Tegeta tumekuja kupata matibabu na kalazwa kwa muda ili afanyiwe vipimo vya MRI, maana leo usiku hajalala kabisa kwani muda wote alikuwa akilalamika tu miguu inamuuma.
“Imefikia wakati hadi nahisi maumivu yake na nabaki nalia tu, nampenda sana mama yangu kiasi kwamba natamani hata ningekuwa na fedha za kutosha kama zamani, hivi sasa ningekuwa nje ya nchi kupata matibabu zaidi, anateseka usiku na mchana,” alisema Ray C.

No comments:

Post a Comment

POSTED TITLE

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...