Sunday, March 15, 2015

ILIBAKI HIVI TU DIAMOND AKATWE MGUU!

Msanii nguli wa muziki wa kizazi kipya na nyota wa Wimbo wa Nitampata wapi aliyewahi kuwa mchumba wa Wema Sepetu, Nasibu Abdul ‘Diamond’ amenusurika kukatwa mguu katika Hospitali ya TMJ, Mikocheni jijini Dar es Salaam kufuatia ugonjwa wa Foot Corn (maarufu kwa jina la kisahani) kumtesa kwa kipindi kirefu.
 
Kwa mujibu wa chanzo chetu makini, Diamond ambaye kwa sasa anaminya kimalavidavi na mwanamama Zarina Hassan ‘Zari’, alianza kusumbuliwa na ugonjwa huo takribani siku 730 zilizopita (miaka miwili), huku mwenyewe akipuuzia matibabu yake na kuelekeza nguvu kwenye shoo za ndani na nje ya nchi.
Msanii nguli wa muziki wa kizazi kipya na nyota wa Wimbo wa Nitampata, Nasibu Abdul ‘Diamond’.

“Mara kwa mara alikuwa akilalamikia maumivu makali ya mguu lakini kwa kuwa yalikuwa yakija na kupotea, alikuwa akipuuzia kwenda hospitali mpaka juzi (Ijumaa) alipoamua kwenda TMJ,” kilisema chanzo chetu kwa masharti ya kutotajwa jina.



WALICHOKIBAINI MADAKTARI
“Madaktari walipompima, walishangazwa na jinsi alivyokuwa amechelewa kwenda kupata matibabu, nasikia ugonjwa aliokuwa nao ni hatari sana. Kama angeendelea kuchelewa, huenda wangelazimika kumkata mguu kabisa, Diamond aliogopa sana,” kilisema chanzo hicho.
Ikazidi kuelezwa kuwa baada ya vipimo kukamilika na kubainika kuwa alikuwa na Foot Corn, madaktari walimueleza kuwa ni lazima wamfanyie upasuaji wa haraka wa kutoa nyama zilizokuwa zimeota kwenye mguu wake ambazo zilitengeneza kitu kama kisahani.

Staa Nasibu Abdul ‘Diamond Platinumz’.
NDANI YA CHUMBA CHA UPASUAJI
Baada ya taratibu zote kukamilika, Diamond aliingizwa ndani ya chumba cha upasuaji ambapo jopo la madaktari kadhaa, wakiwemo wenye asili ya Bara la Asia walimfanyia upasuaji.

SHOO NYINGI ZILISABABISHA ACHELEWE MATIBABU
Kwa mujibu wa chanzo kingine ambacho ni ndugu wa msanii huyo, sababu iliyosababisha Diamond akachelewa kwenda hospitali kutibiwa tatizo hilo, ni kubanwa na shoo nyingi ambapo alikuwa akihofia kwamba akienda hospitali anaweza kulazwa au matibabu yakachukua muda mrefu hivyo kuvuruga mikataba ya shoo ambayo tayarti alikuwa ameshasaini.

MSIKILIZE DIAMOND
Baada ya kukamilika kwa upasuaji huo, mwanahabari wetu aliyekuwa akifuatilia tukio zima kuanzia mwanzo hadi mwisho, alizungumza na Mbongo Fleva huyo ambapo alikuwa na haya ya kusema:
“Nawashukuru sana madaktari wa TMJ kwa kuweza kufanikisha upasuaji huu, Mungu awabariki sana. Ugonjwa ulianza kama miaka miwili hivi iliyopita lakini nilishindwa kufanya upasuaji kwani shoo zilikuwa zinabana, safari hii nikaona bora tu nifanye maana niliambiwa nikiacha tatizo linaweza kuwa kubwa zaidi,” alisema Diamond.

MSIKIE DAKTARI BINGWA WA UPASUAJI
Ijumaa Wikienda halikuishia hapo, lilimtafuta Dk. Edward Wayi, Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Hospitali ya CCBRT ambaye pia huzunguka katika nchi mbalimbali za Afrika kutibu watu ambapo aliufafanua ugonjwa huo kitaalamu.
“Ugonjwa wa Foot Corn unapokuanza, dalili za awali ni maumivu makali ya mguu ulioathirika.
“Ugonjwa usipotibiwa, husababisha malengelenge ambayo hupasuka na kusababisha kidonda. Kidonda hicho kisipotibiwa, husababisha kuharibika kwa ngozi ya ndani ya mguu inayotenganisha mifupa ya mguu na ngozi ya ndani. Hali hii kitaalamu huitwa    Bursitis.

“Mgonjwa akishafikia hatua hii, huwa kwenye hatari ya kupata tatizo lingine kubwa zaidi liitwalo Septic Arthritis ambapo bakteria huingia ndani ya mwili kwa kupitia kidonda, kusambaa kwenye mfumo wa damu na kwenda kujikusanya kwenye viungio vya mifupa (joints).
“Mgonjwa akifikia hatua hii, viungio vya mifupa huvimba na kupata maumivu makali mithili ya mtu anayechomwa na sindano au msumari. Hata hivyo, kwa kuwa maumivu huwa yanakuja na kukata, wengi hupuuzia na matokeo yake, ugonjwa huingia kwenye hatua ya hatari zaidi iitwayo Osteomyelitis.
“Katika hatua hii, bakteria huwa tayari wamepanda na kuingia ndani ya mfupa kisha kuanza kuushambulia kwa kasi.
Mgonjwa akishafikia hatua hii, huwa hakuna tiba nyingine zaidi ya mguu kukatwa. Nawashauri Watanzania kutopuuzia ugonjwa huu kwani tayari watu wengi wameshakatwa miguu kwa sababu ya kuchelewa kupata matibabu,” alihitimisha daktari huyo.

No comments:

Post a Comment

POSTED TITLE

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...