NYOTA wa filamu za Kibongo, Haji Adamu Rajabu ‘Baba
Haji’ amefunguka kuwa, soko la filamu Bongo kwa sasa linashuka siku
hadi siku na sababu kubwa ni wasanii kutopenda kwenda shule
kujiendeleza kielimu na kujua ni jinsi gani filamu inatakiwa
kutengenezwa.
Akizungumza na Risasi Jumamosi, Baba Haji alisema anakubaliana na
kila mtu anayesema soko limeshuka kwa sababu wasanii wanapenda kukopi,
pia hawapendi kuandika miswada ya filamu na kupendelea kuingiza mambo ya
kizungu, ingawa wengi wanamtaja msanii Steven Kanumba kuwa ameondoka
na soko hilo.
Baba haji anafunguka kama hivi…
Risasi Jumamosi: Vipi, mbona kimya kingi? Soko la filamu limekwenda na Kanumba au unalionaje?
Baba Haji: Tunaweza kusema hivyo, kwa sababu yeye alikuwa anajitoa kwa
hali na mali, anatoa pesa zake kwa ajili ya filamu, ni tofauti na
wasanii wengine ingawa pia alikuwa akitumia sana ‘media’ kueleza kila
anachokifanya.
Risasi Jumamosi: Unadhani ni kwa nini wasanii wengi wanapenda kufanya kazi na Wanaigeria?
Baba Haji: Kwa sababu wao wanalipwa tu ila nchi nyingine wana sheria kali, kufanya kwao filamu ni mpaka uwe na digrii ya sanaa.
Risasi Jumamosi: Wewe umejipanga vipi kwa hilo?
Baba Haji: Mimi
nimejipanga vizuri kwa sababu nilikwenda Shule Bagamoyo (Pwani) kwa
muda wa miaka mitatu na nilifanikiwa kupata diploma ya sanaa, wakati
nakwenda shule nakumbuka Kanumba aliniambia napoteza muda kwani soko
ndiyo lilikuwa limechanganya ila namshukuru Mungu hata niliporudi
sijapotea sana kwa mashabiki.
Risasi Jumamosi: Una kipimo gani kinachoonesha hujapotea?
Baba
Haji: Filamu nilizocheza ni nyingi na juzi nimegundua bado nipo baada ya
filamu yangu ya Jamila na Pete ya Ajabu kutoka na kupokelewa na
mashabiki vizuri mpaka wamelibadili jina langu kwa sasa wananiita Baba
Jamila.
Risasi Jumamosi: Matarajio yako ya baadaye ni yapi?
Baba Haji:
Mungu akipenda mwezi wa tisa narudi shule kwa ajili ya kuchukua digrii
ya sanaa ambayo nina uhakika itanipeleka mbali zaidi na nimefanikiwa
kufungua kampuni yangu inayoitwa Hapa Production ambayo imeandaa filamu
yangu ya kwanza ya Mama si Mama itatoka hivi karibuni Mungu akipenda.
Risasi Jumamosi: Unadhani ni kwa nini mnashindwa kupasua anga za
kimataifa zaidi ukiacha ishu ya Kanumba kujitolea pesa zake mfukoni?Baba
Haji: Nawashauri wasanii wajinoe zaidi kwenye lugha ya kigeni kwani na
yenyewe inachangia wao kushindwa kufanya vizuri kwenye soko la
kimataifa.
Risasi Jumamosi: Unaweza kunipatia historia yako fupi ya sanaa tangu ulipoanzia mpaka sasa?
Baba Haji: Nilianza kuigiza 1998, nilianzia kundi lililoitwa Mtanzania
ambalo lilikuwa chini ya Chama cha Mapinduzi (CCM), mwaka 2000 nikaenda
Nyota Academia kundi lililokuwa likiongozwa na mwalimu marehemu George
Otieno ‘Tyson’, mkurugenzi akiwa ni Singo Mtambalike ‘Richie’.
Sikuishia hapo, mwaka 2002 tulianzisha Kundi la Kamanda Family nikiwa
na Richie Mtambalike ambapo tulicheza michezo mbalimbali kisha tukaamua
kuanza kucheza filamu ambapo tulicheza filamu ya Masaa 24 tukaona
filamu ndiyo mpango mzima.
Mwaka 2003 nilicheza filamu ya Miss Bongo niliyoshirikiana na Aunt
Ezekiel, iliyofuata ilikuwa ni Jeraha ya Ndoa, nilicheza na
Monalisa.Mwaka 2004 nilikwenda Bukoba (Kagera) ambapo nilichukuliwa na
Abantu Vision kwa ajili ya kufanya sinema iliyohusiana na mambo ya HIV
ilivyoingia Tanzania. Filamu hiyo ilifanikiwa kuchukua Tuzo ya Ziff kama
Filamu Bora ya mwaka 2005.
Mwaka 2010 nilijiunga na Chuo cha Sanaa Bagamoyo ambapo nilisoma mpaka kumaliza mwaka 2013.
Mwaka 2014 nilifanikiwa kucheza filamu nyingi kama vile Barbara,
Kitoga, Don’t Cry, Mary Mary, Charles Mvuvi, Mwandishi wa Habari, Jamila
na Pete ya Ajabu na Wa Mwisho Wewe.
Mwaka huu ndiyo wa mavuno kwangu kwani nimejiandaa vema kutoa filamu
zangu mwenyewe ambazo zitakuwa na changamoto kubwa kwani nimesoma kwa
ajili ya kuja kuvifanyia kazi na kuibadili kabisa tasnia ya filamu.
No comments:
Post a Comment