Wednesday, September 5, 2012

WAANDISHI WA HABARI WAMLIA NGUMU MANUMBA

 
Wanahabari Iringa wakiwa katika ukumbi wa ofisi ya RPC jana
WAANDISHI wa Habari wa mkoani Iringa wamekataa kupokea taarifa ya awali ya uchunguzi ya mauaji ya mwanahabari Daudi Mwangosi iliyofanywa na jeshi hilo iliyokuwa itolewe jana na Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai (DCI), Robert Manumba.

Hatua hiyo imekuja baada ya Manumba kukataa kuwaondoa katika mkutano wake na waandishi wa habari maafisa wa jeshi la Polisi wanaofanya kazi mkoani hapa huku kukiwepo na tamko la waandishi hao kusitisha kufanya nao kazi ya kihabari mpaka tume huru zilizoundwa zitakapotangaza matokeo ya uchunguzi wao.

Pamoja na wanahabari kukataa kupokea taarifa hiyo, Manumba alikanusha taarifa zingine zinazodai kuwepo kwa waandishi wa habari wawili wanaodaiwa kuwepo katika mpango wa kuuawa na baada ya mmoja wa wanahabari hao Francis Godwin kujisalimisha na kumuhoji sababu za kutakiwa ajisalimishe polisi.

Katika kikao hicho kilichoitishwa majira ya saa sita mchana katika ukumbi wa mikutano uliopo katika ofisi ya Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Iringa, wanahabari walionesha msimamo wao kwa kumtaka Manumba awatoe maafisa wa jeshi hilo wa mkoani hapa.

“Waandishi wa Habari wa Mkoa wa Iringa walikwishatangaza katika tamko lao kwamba wamesitisha ushirikiano wa kihabari na jeshi hilo la Polisi mkoani hapa mpaka pale tume huru zilizoundwa kuchunguza kifo cha mwanahabari huyo zitakapotoa majibu yao,” alisema Frank Leonard ambaye ni Katibu Mtendaji wa Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Iringa.

Leonard alimwambia Manumba kwamba waandishi wa habari hawana tatizo lolote na yeye na kwamba wapo tayari kupokea taarifa yake hiyo ya uchunguzi ila kwa sharti kwamba ni lazima maafisa polisi wote wanaofanya kazi mkoani hapa na ambao walikuwepo katika chumba hicho cha mikutano watoke.

“Huu ni msimamo wetu, hatupo tayari kufanya kazi na maafisa wa jeshi lako na tunamuomba IGP Said Mwema ampumzishe kazi kwa muda Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Iringa bwana Michael Kamuhnada mpaka pale tume huru zilizoundwa zitakapotoa taarifa za matokeo ya uchunguzi wao,” Leonard alisema alipokuwa akitoa ufafanuzi juu ya tamko la wanahabari hao.

Akiwasihi wanahabari kushirikiana na jeshi la Polisi, Manumba alisema mara baada ya mauaji hayo kutokea jeshi la Polisi makao makuu liliunda tume ya uchunguzi akiwemo yeye mwenyewe ambayo kwa kiasi kikubwa imeifanya kazi hiyo.

“Leo nilikuwa nataka niwape taarifa ya uchunguzi ya mauaji hayo, lakini kwa sharti mnalonipa sidhani kama hilo litawezekana,” alisema.

Alisema kila mtu ameguswa na mauji ya Mwandishi huyo na kwamba kosa lililofanywa na wahusika haliwezi kuwa kosa la kila mtu.

Bila kufafanua Manumba alisema matukio ya aina hiyo yapo katika jamii yetu, na yanaweza kuendelea kutokea ikiwa ni pamoja na kwake au maafisa wa jeshi hilo.

“Jambo hili baya limetokea na sisi Polisi tuna regret na hata serikali ina regret, ndio maana tume iliundwa na mara moja tukakimbia kuja hapa ili kupata ukweli baada ya kupeleleza na tukaona ni vizuri uchunguzi tuliofanya tuutoe kwenu” alisema.

“Hata hivyo kwa kuwa huu ni msimamo wa waandishi na wote mmeuunga mkono mbele yangu, nadhani uchunguzi uliofanywa na jeshi letu itabidi upitiwe na tume nyingine badala ya kuutoa kwenu,” alisema.

Hata alipoombwa akatoe taarifa ya uchunguzi huo ambayo hata hivyo baadhi ya wanahabari walisema inaweza kuwa na lengo la kuvuruga ushahidi unaokusudiwa kukusanywa na tume zingine ikiwemo ile iliyoundwa juzi na Waziri wa Mambo ya Ndani, Emanuel Nchimbi, DCI alisema tume iliyoundwa na waziri inatakiwa iachwe ifanye kazi yake kwahiyo itapata fursa pia ya kupitia uchunguzi wao huo.

Katika kipindi hiki kigumu kwa wanahabari na wadau mbalimbali wa tasnia hiyo, Manumba alisema yapo mengi yatakayozungumzwa kuhusu kifo cha Mwangosi zikiwemo taarifa za uzushi, za kupikwa na za ukweli.

Kuhusu kuwepo kwa taarifa ya orodha ya waandishi wahabari wengine wawili wanaotakiwa kushughulikiwa na jeshi hilo, Manumba alisema hazina ukweli kwani mbali na kufanya kazi na wadau wengine, jeshi hilo linawategemea sana wanahabari katika kazi zake.

“Kwahiyo ndugu zanguni mkutano umefungwa na sasa tuiache tume ifanye kazi yake,” alisema.
 
Katibu wa Iringa Press Club Frank Leonard akiwasilisha msimamo wa wanahabari kwa DCI Manumba.
M Francis Godwin akiwa na mkewe wakitoka katika ofisi ya RPC baada ya Manumba kushindwa kufuata msimamo uliotolewa na wanahabari wa Iringa.
 
DCI Robert Manumba akiongea na waandishi Iringa jana
 
Waandishi wa habari wa Iringa wakiwa katika ofisi ya RPC jana

No comments:

Post a Comment

POSTED TITLE

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...