Monday, February 15, 2016

NAY: NAHISI KUUAWA MUDA WOWOTE!

Picha ya Nay wa Mitego iliyoharibiwa na baadhi ya wapinzani wake kwa lengo la kumchafulia jina.
Nyota wa Bongo Fleva, Emmanuel Elibariki ‘Nay wa Mitego’.

Hali ni tete! Siku chache baada ya nyota wa Bongo Fleva, Emmanuel Elibariki ‘Nay wa Mitego’ kuwasiliba wasanii wenzake kwenye wimbo wake mpya wa Shika Adabu Yako, ameibuka akidaiwa kujisalimisha polisi kufuatia kutishiwa kuuawa na watu asiowafahamu.

CHANZO CHAWEKA WAZI
Kwa mujibu wa chanzo chetu, baada ya kuachia wimbo huo, jioni yake tu, Nay alipigiwa simu na watu asiowafahamu wakimtaka aupotezee wimbo huo kabla haujamgharimu maisha kwa njia yoyote ile.

APUUZA, ATUMIWA MESEJI
Chanzo kilidai kuwa, Nay alipuuzia simu hizo lakini alishangaa ilipofika asubuhi siku iliyofuata, alikuta ujumbe wa maneno (SMS) kwenye simu yake ukiwa na maneno makali na ya kuendelea kumtishia kifo.

Picha iliyotengenezwa kumdhalilisha Ney wa Mitego.

INSTAGRAM NI ZAIDI
Chanzo hicho kiliendelea kudai kuwa, Nay, akiwa anafikiria namna ya kukabiliana na vitisho hivyo, aliingia kwenye akaunti yake ya Instagram ‘direct’ (moja kwa moja) na ‘hamadi’ akakutana na ujumbe ukiwa na vitisho vya kumuua.

“Jamaa hana raha hata kidogo, amekutana na meseji na simu alizopigiwa. Ameamua kuzima simu zake zote. kilisema chanzo hicho.“Kwa sasa anajiandaa kwenda mkoani Lindi kuna shoo hivyo tunapata hadi wasiwasi kama jamaa ataweza kweli kufanya kazi inavyotakiwa,” Chanzo.

KWENDA POLISI
Imezidi kudaiwa kwamba, baadhi ya watu wake wa karibu na mama yake mzazi, walimshauri aende akaripoti Kituo cha Polisi Kimara (jirani na nyumbani kwake) kwa vile anaweza kupata matatizo makubwa.

MAMA YAKE ANALIA TU
“Mbaya zaidi, mama yake naye, amepaniki kiasi kwamba analia tu. Inabidi sisi ndiyo tumpe moyo maana anafikiria hatima ya mwanaye kwani kila anapokwenda akikutana na watu wanamlalamikia juu ya wimbo huo,” kilisema chanzo hicho.

Kamanda Simon Sirro.

WIKIENDA LAMSAKA
Baada ya kupenyezewa ubuyu huo, Ijumaa Wikienda lilimtafuta Nay kutaka kujiridhisha kuhusu madai hayo lakini hakuwa hewani. Ilibidi kumtafuta mtu wa karibu yake na ndipo alipopatikana.

Naye alikiri kutishiwa kuuawa. Alisema hatua ya awali alichukua uamuzi wa kwenda Kituo cha Polisi Kimara, Dar lakini hakufunguliwa faili la kesi kwa maelezo kuwa, usiku huo askari wasingeweza kufanya hivyo badala yake walimtaka arudi kesho yake.

HUYU HAPA NAY
“Hapa nilipo nimechanganyikiwa. Kwa hali ilivyo nimeona bora niende polisi maana najua nitauawa wakati wowote. Nilikwenda Polisi Kimara lakini sikufanikiwa, sasa najiongeza, nitakwenda Kituo cha Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam (kwa Kamanda Simon Sirro).

Wikienda: “Nimesikia unakwenda Lindi kwenye shoo, sasa huko Polisi Kanda Maalum umeshakwenda au utakwenda ukirudi?”

Nay: “Kwanza nilikwenda polisi pale Kimara, wakashindwa kufungua faili. Waliniambia niende asubuhi lakini nimeshindwa kwa kuwa nimeondoka Dar na hapa nipo Lindi.

“Ila kuna ujumbe nimeukuta Insta (Instagram) ni mbaya sana. Nimepanga nikirudi nienda Kanda Maalum, lakini kuna wenzangu niliokuja nao hapa Lindi wamenishauri niende Kituo cha Polisi Kikuu cha hapahapa nikaripoti.”

TIMU WEMA WAMFANYA VIBAYA
Wakati huohuo, wadau wa Miss Tanzania 2006, Wema Sepetu (Team Wema), wanadaiwa kuchukua picha ya mrembo huyo akiwa kwenye gari na kuipachika sura ya Nay ili aonekane ni demu.

Kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii, picha hiyo imeenea huku wengi wakikitafsiri kitendo hicho kuwa ni cha kutaka kumdhalilisha Mbongo Fleva huyo aonekane ni shoga.

Katika wimbo huo ulioleta figisufigisu, kuna kipengele Nay alisema Wema hana mimba bali anatafuta kiki ya msimu hali iliyotibua hasira za Team Wema.

No comments:

Post a Comment

POSTED TITLE

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...