Tuesday, June 9, 2015

URAIS 2015 WASANII VIPANDE

MPASUKO! Zikiwa zimesalia takriban siku 31 kabla ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kumpitisha mgombea mmoja wa urais atakayechuana na vyama vya upinzani, imebainika kuwa mastaa wa filamu na Bongo Fleva wamegawanyika vipande huku wakiwa kwenye msuguano mkali kufanikisha ushindi wa makada Bernard Membe na Edward Lowassa, Risasi Mchanganyiko linapa mchapo kamili.
Waziri wa mambo ya nje Bernard Membe.
WAJIPAMBANUA
Taarifa kutoka ndani ya tasnia hizo ambazo zina nguvu ya ushawishi katika jamii zimeeleza kuwa, Membe ambaye ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, kwa kiwango kikubwa amewakamata wasanii wengi wa Bongo Movies wanaomuunga mkono huku Lowassa (Waziri Mkuu wa zamani) akiwa amewadhibiti vilivyo mastaa wa Bongo Fleva.
“Ni mpasuko wa aina yake, Membe ameonekana kuwakamata kisawasawa wasanii wa Bongo Movies na ndiyo maana hata juzi (Jumapili iliyopita), mastaa wengi wa filamu walikwenda Lindi kumuunga mkono alipokuwa anatangaza nia.
Membe akiwa na wasanii wa bongo movie.
WANACHOKIAMINI
“Mastaa kama Steve Nyerere (Steven Mengere, JB (Jacob Steven), Ray (Vincent Kigosi), Dude (Kulwa Kikumba, wanaoonekana katika picha ndogo ukurasa wa kwanza) Hashim Kambi, Ester Kiama (Ester wa Dude) Swebe (Adam Melele) na wengine kibao wameshatonywa kuwa CCM itampitisha Membe hivyo wanamuunga mkono kwa nguvu zote kuhakikisha wanapata sapoti pindi atakapopitishwa na chama chake kisha kuwa rais.

WENGINE HAWAJIPAMBANUI
“Timu ya wasanii wa filamu wanaomuunga mkono Membe ni kubwa sana sema wengine hawajajitokeza hadharani lakini wanapambana chini kwa chini kwani wana uhakikia kwamba piga ua, CCM itampitisha tu.
Waziri mkuu mstaafu Edward Lowassa.
LOWASSA SASA
“Kwa upande wa Lowassa, amepata zaidi mastaa wa muziki. Nao wameamua kujipambanua kwa kuwa nao wametonywa kwamba rais ni Lowassa. Wanaamini hivyo, wanapambana kweli kuhakikisha anachukua mikoba ili aje awatimizie mahitaji yao.
“Utakumbuka wiki chache zilizopita alitangaza nia kule Arusha wasanii kibao wa muziki wakiongozwa na Diamond (Nasibu Abdul), Nay wa Mitego (Emmanuel Elibariki), Khadija Kopa na wengine wengi tu walienda kumuunga mkono. Kuna nyimbo 21 maalum za Lowassa zilizotungwa na wasanii mbalimbali na kusambazwa kama njugu kwa makundi tofauti ya watu wakiwemo waendesha bodaboda.
WAPO WA CHINI KWA CHINI
“Kama ilivyo kwa Membe, Lowassa naye ana timu kubwa sana katika Bongo Fleva ambayo inapambana chini kwa chini. Kuna wasanii kama R.O.M.A (Ibrahim Mussa), Juma Kassim (Nature), Recho (Winfrida Josephat) wote ni Team Lowassa. Yaani uchaguzi wa mwaka huu ni full mpasuko,” zilieleza taarifa hizo.
MBIVU MBICHI, JULAI 12
Kwa mujibu wa ratiba ya chama cha mapinduzi CCM, mgombea wa urais atajulikana Julai 12, mwaka huu mara baada ya kikao cha Mkutano Mkuu kumalizika.
CHANZO: GPL

No comments:

Post a Comment

POSTED TITLE

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...