MPASUKO! Zikiwa zimesalia takriban siku 31 kabla ya
Chama Cha Mapinduzi (CCM) kumpitisha mgombea mmoja wa urais
atakayechuana na vyama vya upinzani, imebainika kuwa mastaa wa filamu na
Bongo Fleva wamegawanyika vipande huku wakiwa kwenye msuguano mkali
kufanikisha ushindi wa makada Bernard Membe na Edward Lowassa, Risasi
Mchanganyiko linapa mchapo kamili.
WAJIPAMBANUA
Taarifa kutoka ndani ya tasnia hizo ambazo zina
nguvu ya ushawishi katika jamii zimeeleza kuwa, Membe ambaye ni Waziri
wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, kwa kiwango kikubwa
amewakamata wasanii wengi wa Bongo Movies wanaomuunga mkono huku Lowassa
(Waziri Mkuu wa zamani) akiwa amewadhibiti vilivyo mastaa wa Bongo
Fleva.
“Ni mpasuko wa aina yake, Membe ameonekana kuwakamata kisawasawa
wasanii wa Bongo Movies na ndiyo maana hata juzi (Jumapili iliyopita),
mastaa wengi wa filamu walikwenda Lindi kumuunga mkono alipokuwa
anatangaza nia.
WANACHOKIAMINI
“Mastaa kama Steve Nyerere (Steven Mengere, JB
(Jacob Steven), Ray (Vincent Kigosi), Dude (Kulwa Kikumba, wanaoonekana
katika picha ndogo ukurasa wa kwanza) Hashim Kambi, Ester Kiama (Ester
wa Dude) Swebe (Adam Melele) na wengine kibao wameshatonywa kuwa CCM
itampitisha Membe hivyo wanamuunga mkono kwa nguvu zote kuhakikisha
wanapata sapoti pindi atakapopitishwa na chama chake kisha kuwa rais.
WENGINE HAWAJIPAMBANUI
“Timu ya wasanii wa filamu wanaomuunga
mkono Membe ni kubwa sana sema wengine hawajajitokeza hadharani lakini
wanapambana chini kwa chini kwani wana uhakikia kwamba piga ua, CCM
itampitisha tu.
LOWASSA SASA
“Kwa upande wa Lowassa, amepata zaidi mastaa wa
muziki. Nao wameamua kujipambanua kwa kuwa nao wametonywa kwamba rais ni
Lowassa. Wanaamini hivyo, wanapambana kweli kuhakikisha anachukua
mikoba ili aje awatimizie mahitaji yao.
“Utakumbuka wiki chache zilizopita alitangaza nia kule Arusha wasanii
kibao wa muziki wakiongozwa na Diamond (Nasibu Abdul), Nay wa Mitego
(Emmanuel Elibariki), Khadija Kopa na wengine wengi tu walienda kumuunga
mkono. Kuna nyimbo 21 maalum za Lowassa zilizotungwa na wasanii
mbalimbali na kusambazwa kama njugu kwa makundi tofauti ya watu wakiwemo
waendesha bodaboda.
WAPO WA CHINI KWA CHINI
“Kama ilivyo kwa Membe, Lowassa naye ana timu kubwa sana katika Bongo
Fleva ambayo inapambana chini kwa chini. Kuna wasanii kama R.O.M.A
(Ibrahim Mussa), Juma Kassim (Nature), Recho (Winfrida Josephat) wote ni
Team Lowassa. Yaani uchaguzi wa mwaka huu ni full mpasuko,” zilieleza
taarifa hizo.
MBIVU MBICHI, JULAI 12
Kwa mujibu wa ratiba ya chama cha
mapinduzi CCM, mgombea wa urais atajulikana Julai 12, mwaka huu mara
baada ya kikao cha Mkutano Mkuu kumalizika.
CHANZO: GPL
No comments:
Post a Comment