Thursday, June 11, 2015

PENNY: MITANDAO ILITAKA KUNITOA UHAI WANGU

Ndani ya safu hii leo tunakutana na Mtangazaji Penniel Mungilwa ‘Penny’ ambaye yuko kimya katika masuala ya utangazaji tangu alipoamua kuondoka Radio E FM.
Mtangazaji Penniel Mungilwa ‘Penny’.
Msikilize Penny alipobanwa kwa maswali kumi na Mwandishi Wetu Imelda Mtema.
Ijumaa: Upo kimya sana shosti, ni nini unachofanya kwa sasa?
Penny: Sasa hivi mimi ni mbunifu wa mpangilio wa nyumba na ofisi ambapo namshauri mtu aiwekeje nyumba yake katika muonekano mzuri wenye mvuto pamoja na ofisi kwa ujumla.
Ijumaa: Mambo ya utangazaji umeachana nayo au una mpango wa kusaka kazi sehemu nyingine?
Penny: Unajua hakuna kitu kizuri kama mtu kuwa na taaluma yako kichwani, yaani hata kama nitakaa miaka kumi bado fani yangu itakuwa ni utangazaji.
Ijumaa: Kuna tetesi kuwa ukikasirishwa tu na mpenzi unakimbilia kunywa sumu, ni kweli?
Penny: (kicheko) Hao wanaosema hivyo watakuwa wananijua sana kuliko mama yangu, siko hivyo wanavyodai jamani.
Ijumaa: Mwanaume ambaye uliamua kumuweka wazi alikuwa ni Diamond tu, kwa nini sasa hivi unaficha?
Penny: Unajua kuna mwanaume mwingine hapendi mambo ya kujulikana kwani wote siyo mastaa.
Ijumaa: Kwa sasa wewe na Wema ni marafiki, je mkikaa huwa hamuongelei mambo ya mpenzi wenu aliyepita?
Penny: Hakuna kitu kama hicho, sisi huongelea mambo yetu binafsi kwani urafiki wetu ni tangu kitambo.
Ijumaa: Kuna kipindi ulivalishwa pete ya uchumba na ulikuwa mbioni kuolewa, ilikuwaje?
Penny: Ni kweli na lengo bado liko palepale, ikifika muda nitaolewa kwani sijatangaza kama tumeachana.
Ijumaa: Kuna kipindi ulikutana na mtihani kupitia mitandao ya kijamii, ulijifunza nini?
Penny: Nilichojifunza ni kwamba watu wengi wanaotumia mitandao ya kijamii wanakurupuka na hawana utu kwani wanaweza kupoteza uhai wa mtu kama hayuko imara.
Ijumaa: Ulishafikiria kutoa uhai wako kwa ajili ya mitandao ya jamii?
Penny: Nilishawahi kuwaza nijiue lakini namshukuru sana mama yangu aliniambia kuwa hakuna kitu ambacho hakiwezi kuisha hata siku moja.
Ijumaa: Unazungumziaje bifu la Kajala na Wema?
Penny: Mimi ninachojua wale ni marafiki wanaopendana sana, ipo siku tofauti zao wataweka pembeni kwa sababu siku hizi hakuna haja ya kuwekeana mabifu.
Ijumaa: Ulishawahi kwenda kwa mganga kwa kusaka mafanikio au jambo lolote?
Penny: Siku zote katika maisha yangu mganga wangu ni Mungu maana ananijibu kwa haraka sana, sijawahi kumtegemea mganga wala hilo halitatokea.

No comments:

Post a Comment

POSTED TITLE

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...