Friday, April 3, 2015

MALI ZILIZOMZIMISHA GWAJIMA!

KWA wiki moja sasa, baadhi ya vyombo vya habari vimekuwa vikiripoti kwamba, kujisikia kizunguzungu hatimaye kuanguka na kupoteza fahamu kulikomtokea Mchungaji wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima wakati akihojiwa na polisi kulitokana na kuulizwa maswali yaliyohusu namna alivyozipata mali zake.
Mchungaji wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima.
Machi 28, mwaka huu Mchungaji Gwajima alipojisalimisha Kituo Kikuu cha Polisi Kanda Maaalum ya Dar es Salaam kwa madai ya kumtolea maneno yenye kuudhi Askofu wa Kanisa la Romani Katoliki Jimbo Kuu la Dar, Mwadhama Polycarp Kadinali Pengo, alijikuta akizidiwa ghafla na kukimbizwa Hospitali ya TMJ kwa matibabu huku akiwa amepoteza fahamu.
Ilidaiwa kuwa, Gwajima alipokwenda kituoni hapo kujisalimisha alitarajia kukutana na mahojiano ya kuhusu kauli yake ya kumkashifu Kadinali Pengo, lakini matokeo yake akakumbana na maswali ya kuhusu mali zake.
WALIVYOSEMA WATU
“Unajua Gwajima yeye alipoambiwa ajisalimishe Central kwa kumkashifu Pengo alijua akifika pale ataulizwa kwa nini ulimtusi Pengo? Alikukosea nini? Huoni kama yule ni mtu mzima kuliko wewe? Je, uko tayari kumwomba radhi? Lakini matokeo yake katikati ya maswali akaulizwa mali alizonazo alizipata kwa njia gani?”
KWA NINI ALIZIMIA SASA?
Gari lake la kifahari.
“Sasa suala siyo kwamba swali hilo la kuhusu mali lilikuwa na shida kwake, bali lilikuwa la ghafla ndiyo maana akajikuta akichanganyikiwa na kupoteza fahamu,” kilisema chanzo kimoja.“Wengi wanasema alipoulizwa kuhusu mali alizimia kwa sababu mali zenyewe si halali, hapana! Zile mali ni halali kabisa ila swali halikuwa kwenye mawazo ya Gwajima,” kiliendelea kusema chanzo.

RISASI JUMAMOSI LAZICHIMBA
Kufuatia madai hayo, Risasi Jumamosi liliamua kuzama kazini na kuzichimba mali hizo kwa nia ya kuzitambua ambapo uchunguzi wa kina uliofanywa ulibaini kwamba, Mchungaji Gwajima anamiliki gari la kifahari aina ya Hummer 2 ambalo gharama ya manunuzi mpaka kufika Tanzania ni wastani wa shilingi milioni 250.
Mbali na gari hilo la kifahari, Gwajima amewanunulia wachungaji wake 30 magari ya kutembelea ili kupambana na tatizo la usafiri jijini Dar.
Nyumba yake ya kifahari.
MAGARI YAANIKWA
Baadhi ya magari hayo ni Subaru Forester (sokoni linauzwa shilingi milioni 17), Mitsubishi Pajero (shilingi milioni 16), Toyota Spacio new model (milioni 20) na Toyota Harrier Lexus (milioni 35).
MJENGO WA MAANA
Risasi Jumamosi lilibaini pia kuwa, mchungaji huyo anaishi kwenye  nyumba yake ya kifahari ya ghorofa nne iliyopo   Mbezi Beach, jijini Dar es Salaam.
Helkopta yake.
MABASI 20
Kweli Gwajima ni tajiri kwani Risasi Jumamosi likabaini kuwa, pia anamiliki mabasi 20 ambayo ni kwa ajili ya kuwabeba waumini wa kanisa lake wakati wa kwenda kwenye ibada na kurudi makwao katika sehemu mbalimbali za Jiji la Dar. Mabasi hayo kila moja alilinunua kwa shilingi milioni mia moja na ishirini.
PIA KUNA HELKOPTA
Pia, miezi ya hivi karibuni, Gwajima alinunua helkopta (chopa) kwa ajili ya kuzungukia sehemu mbalimbali nchini kutoa huduma ya kiroho. Uzinduzi wa helkopta hiyo ulifanywa na mbunge wa Monduli (CCM) na waziri mkuu wa zamani, mheshimiwa Edward Lowassa.
Magari ya wachungaji.
ANAONGOZA KWA KUWA NA WAUMINI WENGI
Uchunguzi pia ulibaini kwamba, Kanisa la Mchungaji Gwajima linaongoza kwa kuwa na waumini wengi ambapo wanakadiriwa kufikia 70, 000. Kwa maana hiyo sasa, kama waumini wake watatoa sadaka ya Jumapili kila mmoja kwa shilingi elfu mbili, atakuwa anaingiza shilingi milioni 140 kwa ibada moja.Kwa mwezi, Gwajima atakuwa anaingiza shilingi milioni 560 japokuwa wapo waumini inadaiwa hutoa hadi shilingi laki tano (500,000) kama sadaka kwa ibada moja.
MSAMAHA WA KODI
KWA mujibu wa sheria za nchi, baadhi ya taasisi zimepewa msamaha wa kodi wakati wa kuingiza bidhaa mbalimbali nchini, hasa zinazohusu huduma kwa jamii. Bidhaa hizo ni pamoja na magari (Tax Exemption).
Taasisi hizo ni pamoja na za dini, elimu, afya (madaktari) na nyingine zenye kuhudumia jamii.

Magari ya kubebea waumini.
“Kwa hiyo Gwajima anaweza kumiliki mali nyingi kwa sababu anao msamaha wa kodi, anaweza kuingiza magari mengi kwa kodi ndogo sana,” alisema mmoja wa waumini wa Kanisa la Gwajima.
MKEWE ANASEMAJE?
Kwa mujibu wa mke wa Gwajima, Grace alipozungumza na vyombo vya habari hivi karibuni, alisema suala la mumewe kuzimia waulizwe polisi.“Mume wangu aliondoka mzima kabisa, polisi ndiyo waulizwe kwa nini alizimia.”

No comments:

Post a Comment

POSTED TITLE

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...