Na Erick Evarist
Zikiwa zimebaki siku 218 kufikia Oktoba 20, siku ya uchaguzi mkuu wa
Rais na Wabunge ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), mgombea wa urais
kupitia chama hicho bado ni kitendawili.
Kitendo cha CCM kuchelewesha kupiga kipyenga cha kuanza kwa mbio
hizo, kimepandisha homa kali ya uchaguzi miongoni wa Watanania, huku
kambi za waonesha nia mbalimbali zikiendelea kuundwa na kuimarishwa,
wapambe wakihama kutoka kambi moja kwenda nyingine.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili umebaini kuwa pamoja na waonesha
nia kuwa wengi, kambi zenye nguvu ndani ya chama cha mapinduzi
zinazooneshana ubabe kila siku ni za makada wawili wakongwe wa chama
hicho, Waziri Mkuu wa Zamani, Edward Ngoyai Lowassa na Waziri wa Mambo
ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe.
Taarifa za uhakika kutoka ndani ya chama hicho zinadai kuwa kambi za
wawili hao kadri siku zinavyozidi kusonga zimekuwa katika mapambano
makali na zikibuni kila aina ya mbinu ili kuhakikisha zinajiimarisha na
kutunisha misuli itakayoweza kuwashawishi wajumbe wa Kamati Kuu (CC),
Halmashauri Kuu (NEC) na Mkutano Mkuu kupitisha jina lake.
Kada Lowassa ambaye jina lake linatamkwa sana midomoni mwa watu
anapigana kwa staili ya ‘juu ya ardhi’ huku usiku na mchana akijenga
hali kukubalika na wananchi kuliko wagombea wenzake ili kupata nguvu
kubwa ya kukitishia chama chake kisithubutu kulikata jina lake, iwapo
kuna vigogo ndani ya chama chake wana mpango wa kufanya hivyo.
Mtindo huu wa Lowassa umemfanya aonekane ndiye mwenye mvuto zaidi kwa
wananchi kuliko wagombea wenzake, hasa pale vinapojitokeza vikundi vya
watu mbalimbali wakimshawishi achukie fomu kugombea urais, wakati yeye
mwenyewe hajatangaza nia.
Wakati Lowassa akitumia mtindo wa juu ya ardhi, Kada Membe anadaiwa
kutumia mtindo wa nyambizi wa kwenda chini ya maji bila kuonekana, kambi
yake ikifanya kazi kimya kimya usiku na mchana ili itakapoibuka mbele
ya safari iishangaze kambi ya Lowassa kwa jinsi atakavyokuwa na nguvu,
ingawa kwa mtindo wake wa kupambana hivi sasa watu wengi wanaona kama
hana mvuto.
Mtindo mwingine wa kupambana unaotumiwa na kambi hizi ni
wakupandikiziana ‘wapelelezi’, wapo watu wanaomuunga mkono Membe lakini
hutumika kutoa taarifa kwenye kambi ya Lowassa na wapo walio katika
kambi ya Lowassa ambao hutoa taarifa kwa kambi ya Membe.
Chanzo kingine ndani ya chama hicho kimekazia kuwa kuna baadhi ya
wagombea wa urais wanaotajwatajwa, wamejitokeza lakini kila mmoja ana
mgombea wake (kati ya Lowassa au Membe) ili pindi jina la mmoja kati ya
wawili hao litakapopitishwa, waunganishe nguvu kwa mgombea huyo kwa
ahadi za kupewa madaraka.
“Kuna baadhi ya wagombea wanafuata tu mkumbo ili atakapopita mtu
wake, anawachukua watu wake na kuwaunganisha kwa mtu huyo aliyepita,”
kilisema chanzo hicho.Hata hivyo mitindo hii ya ‘juu ya ardhi’ na
‘nyambizi’ inayotumiwa na kambi za makada hawa wawili, wenye nafasi
kubwa ya kupitishwa na chama chao kugombea urais, inafanya iwe ni kazi
ngumu sana kujua ni nani mbabe kati yao.
Wachambuzi wa mambo ya siasa wanadai kitakachothibitisha nani ni
mbabe ni kipyenga cha mwisho baada ya vikao vya juu vya maamuzi ya Chama
Cha Mapinduzi kupitisha jina moja.
No comments:
Post a Comment