Thursday, March 26, 2015

LOWASSA VS MEMBE NANI MBABE?

Na Erick Evarist
Zikiwa zimebaki siku  218 kufikia Oktoba 20, siku ya uchaguzi mkuu wa Rais na Wabunge ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), mgombea wa urais kupitia chama hicho bado ni kitendawili.
Waziri Mkuu wa Zamani, Edward Ngoyai Lowassa.
Kitendo cha CCM kuchelewesha kupiga kipyenga cha kuanza kwa mbio hizo, kimepandisha homa kali ya uchaguzi miongoni wa Watanania, huku kambi za waonesha nia mbalimbali zikiendelea kuundwa na kuimarishwa, wapambe wakihama kutoka kambi moja kwenda nyingine.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili umebaini kuwa pamoja na waonesha nia kuwa wengi, kambi zenye nguvu ndani ya chama cha mapinduzi zinazooneshana ubabe kila siku ni  za makada wawili wakongwe wa chama hicho, Waziri Mkuu wa Zamani, Edward Ngoyai Lowassa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe.

Taarifa  za uhakika kutoka ndani ya chama hicho zinadai kuwa kambi za wawili hao  kadri siku zinavyozidi kusonga zimekuwa katika mapambano  makali na zikibuni kila aina ya mbinu ili kuhakikisha zinajiimarisha na kutunisha misuli itakayoweza   kuwashawishi wajumbe wa Kamati Kuu (CC), Halmashauri Kuu (NEC) na Mkutano Mkuu kupitisha jina lake.
Kada Lowassa ambaye jina lake linatamkwa sana midomoni mwa watu anapigana kwa staili ya  ‘juu ya ardhi’  huku  usiku na mchana  akijenga hali kukubalika na wananchi  kuliko wagombea wenzake ili kupata nguvu kubwa ya kukitishia chama chake kisithubutu kulikata  jina lake,  iwapo kuna vigogo ndani ya chama   chake wana mpango wa kufanya hivyo.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe.
Mtindo huu wa Lowassa umemfanya aonekane ndiye mwenye mvuto zaidi kwa wananchi kuliko wagombea wenzake, hasa pale vinapojitokeza vikundi vya watu mbalimbali wakimshawishi achukie fomu kugombea urais, wakati yeye mwenyewe hajatangaza nia.
Wakati Lowassa akitumia mtindo wa juu ya ardhi, Kada Membe anadaiwa kutumia mtindo wa nyambizi wa kwenda chini ya maji bila kuonekana, kambi yake ikifanya kazi kimya kimya usiku na mchana ili itakapoibuka mbele ya safari iishangaze kambi ya Lowassa kwa jinsi atakavyokuwa na nguvu, ingawa kwa mtindo wake wa kupambana hivi sasa watu wengi wanaona kama hana mvuto.
Mtindo mwingine  wa kupambana unaotumiwa na kambi hizi ni wakupandikiziana ‘wapelelezi’, wapo watu wanaomuunga mkono Membe lakini hutumika kutoa taarifa kwenye kambi ya Lowassa na wapo walio katika kambi ya Lowassa ambao hutoa taarifa kwa kambi ya Membe.
Chanzo kingine ndani ya chama hicho kimekazia kuwa kuna baadhi ya wagombea wa urais wanaotajwatajwa, wamejitokeza lakini kila mmoja ana mgombea wake (kati ya Lowassa au Membe) ili pindi jina la mmoja kati ya wawili hao litakapopitishwa, waunganishe nguvu kwa mgombea huyo kwa ahadi za kupewa madaraka.
“Kuna baadhi ya wagombea wanafuata tu mkumbo ili atakapopita mtu wake, anawachukua watu wake na kuwaunganisha kwa mtu huyo aliyepita,” kilisema chanzo hicho.Hata hivyo mitindo hii ya  ‘juu ya ardhi’ na ‘nyambizi’ inayotumiwa   na kambi za makada hawa  wawili, wenye nafasi kubwa ya kupitishwa na chama chao kugombea urais, inafanya iwe ni kazi ngumu sana kujua ni nani mbabe kati yao.
Wachambuzi wa mambo ya siasa wanadai kitakachothibitisha nani ni mbabe ni kipyenga cha mwisho baada ya vikao vya juu vya maamuzi ya Chama Cha Mapinduzi kupitisha jina moja.

No comments:

Post a Comment

POSTED TITLE

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...