Monday, February 2, 2015

JEMBE LA CHELSEA LATUA MAN U, HUMMELS NDANI!


Manchester United ipo katika harakati kambambe za kuhakikisha leo inanasa saini ya nyota wawili kwa vyovyote  kabla ya kufungwa kwa dirisha la usajili mdogo leo usiku majira ya saa sita usiku.
Man U inataka kufanya kila linalowezekana kuhakikisha inamnasa kiungo wa zamani wa Chelsea, Kelvin De Bruyne ambaye anakipiga Wolfsburg ya Ujerumani, huku pia ikimuwinda kwa udi na uvumba, beki mahiri wa Borussia Dortmund, Mats Hummels.
Licha ya Bruyne kushindwa kung’ara Stamford Bridge msimu uliopita na kupelekwa Ujerumani, kiwango chake kimekuwa juu ambapo amekuwa nguzo wa Wajerumani hao huku juzi akiiongoza timu yake kuichapa Bayern Munich mabao 4-1, ukiwa ni mchezo wa kwanza kwa Munich msimu huu kati ya mechi 18 ilizoshuka dimbani mpaka sasa.
Van Gaal anaamini kumpata kiungo huyo raia wa Ubelgiji, kutasaidia kwa kiasi kikubwa kuimarisha safu ya kiungo hususan katika mfumo wa 4-4-2 diamond (kupanua uwanja). 
Katika kukamilisha hilo, Van Gaal ametenga kiasi cha pauni milioni 30.
Wakati huohuo, kocha huyo ametamka kuwa anahitaji huduma ya beki wa Dortmund, Hummels licha ya kukiri itakuwa ngumu kumpata kutokana na klabu yake kutokuwa tayari kumuachia katika kipindi hiki ambacho inapigana kujiokoa isishuke daraja katika ligi kuu nchini Ujerumani.
Dortmund ambao ni mabingwa wa msimu 2012/13 wapo mkiani mwa ligi na kocha Jurgen Klopp anapigana kuhakikisha timu hiyo haishuki daraja.
Katika kukamilisha dili hilo, Man U imemtengea kitita cha pauni milioni 37.
Duru za habari nyingine zinasema kuwa Man U wamemfungia kazi beki tegemeo wa Paris Saint Germain (PSG) Marcos Correa ‘Marquinhos’ kwa kutenga kitita cha milioni 35 kama watamkosa Hummels.

No comments:

Post a Comment

POSTED TITLE

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...