Thursday, March 13, 2014

TFDA YAWAFANYIA UKATILI WATUMIA MIKOROGO,YATEKETEZA VIPODOZI VYA THAMANI YA TSH.188



Afisa Uhusiano wa Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA), Gaudensia Simwanza, akionesha moja ya vipodozi vilivyopigwa marufuku na mamalaka hiyo kinachotumiwa na wanawake kukuza makalio.

Baadhi ya vipodozi vilivyopigwa marufuku na Mamalaka ya Chakula na Dawa (TFDA).

Baadhi ya wanahabari wakimsikiliza Afisa Uhusiano wa Mamalaka ya Chakula na Dawa (TFDA), Gaudensia Simwanza (hawapo pichani). Picha na Hussein Makame-MAELEZO.


Frank Mvungi-Maelezo


MAMLAKA ya Chakula na Dawa (TFDA) imeteketeza vipodozi visivyofaa kwa matumizi ya binadamu vyenye thamani ya takribani Shilingi Milioni 188 katika kipindi cha mwaka 2012/2013.


Hayo yamesemwa na Afisa Uhusiano wa mamlaka hiyo, Gaudensia Simwanza wakati akizunguza na wanahabari kwenye mkutano na waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam.


Alisema TFDA imeweka mfumo thabiti wa udhibiti wa vipodozi ambao unatumia njia mbalimbali ambazo ni pamoja na usajili wa vipodozi, utoaji wa vibali vya biashara ya bidhaa husika na ukaguzi wa majengo ya vipodozi.


Simwanza aliongeza kuwa hatua nyingine ni ufuatiliaji wa vipodozi katika soko ili kujiridhisha kuwa vina ubora na usalama unaotakiwa kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizowekwa.


Alibainisha kuwa vipodozi ambavyo havifai kwa matumizi ya binadamu vina madhara kama vile kusababisha kupata mzio wa ngozi, kusababisha ugonjwa wa ngozi kwa mtumiaji.


“Matumizi ya vipodozi vyenye viambata vya zebaki (mercury) kwa mama wajawazito huathiri mtoto tumboni hali inayoweza kusababisha madhara makubwa kwa mtoto atakayezaliwa.


Alifafanua zaidi kuwa viambato kama Zirconium na Vinyl Chloride husababisha kansa ya ngozi na mapafu kwa mtumiaji wa vipodozi vyenye kemikali.


Simwanza alitoa wito kwa wananchi kuchukua tahadhari kwa kuacha matumizi ya vipodozi vyenye viambata vyenye sumu na kemikali.


TFDA imekuwa ikifanya operesheni na ukaguzi wa vipodizi katika maduka mbalimbali yanayouza bidhaa hizo na kukamata bidhaa zisizofaa kwa matumizi ya binadamu na kuziteketeza kwa mujibu wa sheria.

No comments:

Post a Comment

POSTED TITLE

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...