Monday, July 22, 2013

WATOTO WAWILI WABAKWA NA BABA ZAO JIJINI DAR



Ukatili wa kutisha umewakuta watoto wawili wa familia tofauti wakidaiwa kubakwa na wazazi wao huku mmoja akifanyiwa unyama huo na baba yake mzazi na mwingine baba yake mdogo.

Habari zilizopatikana kutoka kwa ndugu, wazazi na majirani wa watoto hao zilisema kuwa wote walifanyiwa ukatili huo siku moja kwa nyakati na mazingira tofauti wilayani Temeke, Dar hivi karibuni.

Watoto hao ambao wote walifikishwa siku moja katika Hospitali ya Wilaya ya Temeke kwa matibabu, walieleza jinsi walivyotendewa unyama huo wa kusikitisha ambao mzazi au mlezi hapaswi kumtendea mwanaye.

Wakwanza ni Anifa (8) ambaye alieleza kuwa alibakwa na baba yake mdogo aliyemtaja kwa jina moja la Amani.
Wapili ni Prisca ambaye alimweleza mwanahabari wetu kuwa alibakwa na baba yake mzazi aliyemtaja kwa jina moja la Charles.

Wakizungumza na mwandishi wetu kwa nyakati tofauti wakiwa wodini hospitalini hapo wakiuguzwa majeraha, watoto hao waliokuwa sambamba na mama zao, walieleza kwa kina kile walichofanyiwa na wazazi wao.

Anifa alisema mara nyingi baba yake mdogo alikuwa akimpa pipi na akimuonesha muvi za picha za utupu na kumshawishi wafanye uchafu huo.

“Kuna wakati alikuwa akiniambia atanipa pesa lakini pia alinitisha kwa kisu au panga ili nimpe, nikawa nakataa lakini siku hiyo usiku alinibaka huku amenishikia kisu,” alisema mtoto Anifa kwa huzuni.

Kwa upande wake, Prisca alisema baba yake alimwambia atampa pesa ili wafanye mapenzi na wakati anamwingilia alikuwa ameshika noti ambayo hata hivyo alishindwa kusema ilikuwa na thamani gani.

Moja kati ya mambo yaliyoibua maswali ni kama kweli wabakaji wa watoto hao ni baba zao?

Ili kupata majibu mwandishi wetu alizungumza na watoto hao kwa kina juu ya ukweli kama wahusika wanawafahamu vizuri ambapo katika mahojiano hayo yaliyorekodiwa, kila mmoja alikiri kuwa wanawajua fika wazazi wao hao.

Bila kupepesa macho wala kuogopa, mtoto Anifa alikiri kuwa mbakaji wake ni baba yake mdogo ambaye mara nyingi alikuwa akimtishia ili afanye naye mapenzi bila mafanikio hadi siku aliyopata nafasi usiku.

Kilichowashangaza wengi ni umri mdogo wa watoto hao kwani mtoto Anifa ana miaka nane huku mwenzake akiwa na umri wa miaka mitano.

“Mwanangu ana miaka mitano tu, sasa najiuliza huyu baba yake alikuwa anatafuta nini kwake, kwa kweli imeniuma sana na nimechanganyikiwa kwa kitendo alichofanyiwa na baba yake,” alisema mama wa Prisca huku mama wa Anifa akithibitisha umri wa mtoto wake kuwa ni miaka minane akiwa ni denti wa darasa la tatu katika shule ya msingi (jina kapuni).

Mama mzazi wa Prisca aliyejitambulisha kwa jina moja la Maria, alisema alishitushwa na taarifa za mumewe kumbaka mtoto wao.

“Nimeshaachana na mume wangu na sasa ameoa mwanamke mwingine, kwa kweli niliumia sana baada ya kupata habari za mwanangu kubakwa na baba yake.

“Nilikwenda Polisi Chang’ombe (Dar) nikamfungulia jalada la kesi namba CHA/RB/6028/2013-UBAKAJI ambapo mtuhumiwa alikamatwa na sasa yupo mahabusu katika Gereza la Keko akisubiri kesi yake kusikilizwa,” alisema mzazi huyo.

Kwa upande wa Anifa, shangazi yake aitwaye Wamoja alisema kuwa mtuhumiwa wa ubakaji wa Anifa alikamatwa mara alipokwenda hospitalini hapo kwa ajili ya kumjulia hali mgonjwa.

“Alijifanya hajui chochote akaja hospitali kwa kuwa Anifa alishamtaja kule polisi, ndipo akakamatwa na kufikishwa polisi Chang’ombe akisubiri kufikishwa mahakamani,” alisema Wamoja.

Baadhi ya mashuhuda wa matukio hayo, walishangazwa na madai ya watoto hao kubakwa na wazazi wao ambapo walisema kuwa siyo bure, lazima kuna kitu nyuma ya pazia.

No comments:

Post a Comment

POSTED TITLE

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...