Wednesday, July 8, 2015

WEMA AGUNDULIKA NA GONJWA LA AJABU

Musa Mateja
Habari mbaya ikufikie kuwa Mkurugenzi wa Kampuni ya Endless Fame Films Productions ambaye yupo kwenye harakati za kuwania Ubunge wa Viti Maalum kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM) mkoani Singida, Wema Isaac Sepetu amegundulika kuwa na gonjwa la ajabu linalomsababishia kukosa raha ambalo linakua kadiri siku zinavyosonga.
Staa wa filamu Bongo, Wema Isaac Sepetu.
Gonjwa hilo limegundulika hivi karibuni machoni mwa paparazi wetu baada ya kumuona mlimbwende huyo wa Tanzania mwaka 2006 akiwa na bonge la nundu nyuma ya shingo, jambo lililomfanya paparazi ashindwe kujizuia na kuamua kumuuliza Wema.
MIAKA 26 MWILINI
Bila kupepesa macho Wema alisema kuwa ‘uvimbe’ huo upo mwilini mwake kwa zaidi ya miaka 26 sasa na umekuwa ukiongezeka siku hadi siku.
Wema alilazimika kufunguka zaidi baada ya paparazi wetu kumuona sehemu hiyo ikiwa imemvimba bila kujua kama ni tatizo lake la miaka yote.
Sehemu ya shingo iliyoonekana kuvimba.
HATA MAMA YAKE?
Wema alitolea ufafanuzi jambo hilo kwa kusema kuwa huo si uvimbe bali ni nundu ambayo amekuwa nayo tangu mwaka mmoja baada ya kuzaliwa na hata mama yake mzazi, Miriam Sepetu pia yuko hivyo.“Huu siyo uvimbe mpya, ujue mimi niko hivi na hii nundu ipo siku nyingi, sema imekuwa ikiongezeka kadiri siku zinavyosonga.
LAMKOSESHA RAHA
“Kweli tatizo hili linanikosesha raha. Nimekuwa nikisuka nywele ndefu na mara nyingine mawigi yangu ni marefu hivyo watu huwa hawanigundui.“Nadhani hili ni tatizo la kifamilia maana mama yangu pia yuko hivihivi isipokuwa mimi linaonekana kuwa kubwa sana,” alisema Wema.
MTU WA KARIBU
Paparazi wetu aliendelea kuchimba kwa watu wa karibu wa Wema ili kujua kama ni kweli hiyo nundu ipo siku zote au alipata ajali, jambo ambalo lilikuwa hivyo kutokana na majibu ya Petit Man ambaye alisema kuwa wao hata hawamshangai tena Wema maana hiyo nundu ipo kitambo na kuna muda huwa wanamtania kwa kumuita jina la Kinundu.
“Haaa! Wewe ulikuwa hujui kama Wema ana nundu, mbona ipo siku nyingi tu, sema huwa anaifunika na nywele na ndiyo maana haionekani sana, muda mwingi watu wamekuwa hawaigundui kwa kuwa ipo nyuma ya shingo, labda ingekuwa mbele au pembeni nadhani kila mtu angekuwa anaiona,” alisema Petit Man.
DAKTARI AFAFANUA
Akizungumza na gazeti hili, daktari maarufu jijini Dar, Godfrey Chale ‘Dokta Chale’ alifafanua kwamba ugonjwa huo kitaalam unajulikana kwa jina la Lipoma na huwa ni mkusanyiko wa nyama ya mafuta kwa ndani hivyo ukubwa wake ukizidi huwa ni gumu.
“Uvimbe huo ukishakuwa na ugumu huo unaotokana na kuwa kubwa husababisha mishipa ya damu kugandamizwa, hali inayomsababisha mgonjwa kuumwa na kichwa kwa upande wa nyuma.
“Pia huaribu muonekano wa kawaida wa mtu,” alisema Dk. Chale na kuongeza:
“Inabidi Wema amuone daktari kwa vipimo na upasuaji ili kuondoa uvimbe huo.”

No comments:

Post a Comment

POSTED TITLE

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...