Friday, February 28, 2014

SPORTS! TFF YASITISHA MKATABA WA KOCHA KIM POULSEN



                                                   Timu ya Taifa ya Tanzania

Hatimaye Shirikisho la Kabumbu nchini Tanzania TFF limetangaza kuvunja mkataba wake na Kocha mkuu wa Timu ya taifa ya soka ya Tanzania Taifa Stars Kim Poulsen kwa kile kilichoelezwa maafikiano ya pamoja baina ya kocha huyo,TFF, na Serikali.
Jamal Malinzi ambaye ni Rais wa Shirikisho la soka Tanzania amesema kuwa huo ni utaratibu wa kawaida hasa baada ya wadau mbali mbali kuona kuwa huu ni wakati wa kufanya mabadiliko ya lazima katika benchi la ufundi la Taifa Stars ambayo inajiandaa kwa mechi za kufuzu kwa Fainali za kombe la mataifa Afrika hapo mwakani zitakazofanyika nchini Morocco.
Kuhusu gharama za kuvunja mkataba na Kocha huyo Bwana Malinzi amesema serikali haitagharamia uvunjaji huo wa mkataba na kocha huyo na badala yake wapo wadau waliojitokeza kugharamia kutokana na kuona umuhimu wa kufanya mabadiliko katika kipindi hiki kwa faida ya soka la Tanzania.
Kwa Upande wake Kocha Kim Poulsen amesema na rekodi yake inaonyesha kuimarika kwa soka la Tanzania katika kipindi cha takriban miaka miwili aliyokuwa akikinoa kikosi cha Taifa Stars lakini kusitishwa mkataba ni jambo la kawaida kwa kocha yeyote baada ya kipindi fulani kutoka sehemu moja na kwenda sehemu nyingine na ndiyo sehemu ya maisha.
“Kama kocha unapoona ndiyo umefanya kazi yako,unapaswa kuangalia mbele zaidi baada ya kufanya kazi yako si lazima uendelee kuwa hapo, mnakaa na kujadiliana na kuachana kwa amani kisha unapaswa kusonga mbele,ninaondoka nikiwa najivunia kipindi nilichofundisha soka hapa,na ninawatakia kila la kheri Tanzania na Taifa Stars kwa ujumla.”alisema Poulsen.
Kuhusu Kocha mpya wa Taifa Stars Jamal Malinzi ambaye ni Rais wa TFF amesema hadi sasa wapo makocha watatu raia wa Uholanzi ni wawili na Mjerumani mmoja wanaosailiwa kwa ajili ya kumrithi Kim Poulsen,lakini moja ya vigezo Malinzi amesema kuwa ni lazima kocha huyo awe amewahi kuipeleka kwenye fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika moja ya nchi zilizoko kusini mwa jangwa la Sahara.
Katika hatua nyingine kocha Salum Madadi ameteuliwa kukaimu nafasi iliyoachwa wazi na Kim Poulsen ambapo kocha huyo akisaidiwa na Hafidh Badru kutoka Zanzibar watasimamia Taifa Stars kwenye mechi ya kirafiki dhidi ya Namibia iliyoko kwenye kalenda ya FIFA baadaye mwezi ujao.

No comments:

Post a Comment

POSTED TITLE

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...