Wednesday, November 27, 2013

MTOTO ARUDISHA PENZI LA MONALISA NA TYSON



NDOA ya mastaa wa filamu Bongo, George Tyson na Yvonney Chery ‘Monalisa’ iliyovunjika kitambo, ilirejewa na uhai wa saa kadhaa katika shughuli ya kumpongeza binti yao mpendwa Sonia baada ya kupata kipaimara.

Mwandishi wetu aliwashuhudia wawili hao wakionekana dhahiri kuweka tofauti zao pembeni na kujali shughuli ya binti yao iliyofanyika Jumapili iliyopita nyumbani kwa mama mzazi wa Monalisa, Suzan Lewis ‘Natasha’, Yombo –Buza, Dar.

Muda wote walionekana wenye furaha na waliketi kwenye meza moja huku Monalisa akionesha heshima wakati wa kumlisha keki Tyson kwa kupiga magoti.

“Hawa jamani wanapendezana sana wakiwa pamoja. Jamani... mtoto wao amerudisha penzi lao. Ingefaa wakafikiria upya na kuona kuna umuhimu wa kurudiana na kumlea pamoja mtoto wao,” mmoja wa wageni waalikwa alisikika akisema.

Katika kuonesha kuwa kweli hawana bifu, Mona aliamua kumtunza mzazi mwenzake noti nyingi za elfu kumikumi zilizokadiriwa kuwa zaidi ya 200,000 ambapo alisema: “Huwa nawashangaa watu wengi wakiwatuza akina mama kwa kuwalea vyema watoto lakini wanawasahau akina baba. Sasa mimi namzawadia baba Sonia kwa sababu bila yeye, mtoto wetu asingekuwepo.”

Tukio hilo lilivuta hisia za watu na kusababisha shangwe kubwa kuibuka katika sherehe hiyo.

No comments:

Post a Comment

POSTED TITLE

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...