Wednesday, September 4, 2013

JWTZ YAWANASA MABOSI WANNE WANYARWANDA


Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Jenerali Davis Mwamunyange.

*Yakamata maofisa wake wanne wa Kijeshi
*M-23 wakiri majeshi ya UN ni hatari yatawamaliza

ASKARI wa Umoja wa Mataifa wanaolinda amani nchini Kongo (Monusco), wakiongozwa na vikosi vya Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), wamedai kuwakamata maofisa wanne wa jeshi la Rwanda, katika mapigano ya wiki iliyopita nchini Kongo.

Akizungumza na MTANZANIA Jumatano kwa sharti la kutotajwa jina, mmoja wa askari aliyepo ndani ya kikosi cha JWTZ huko nchini Kongo, alisema maofisa hao wanashikiliwa kwa mahojiano zaidi.

Taarifa hizi za sasa zinakuja wakati ambapo kumekuwa na madai ya muda mrefu, ambayo yamekuwa yakitolewa na Umoja wa Mataifa pamoja na Marekani kwamba, Rwanda imekuwa ikiwasaidia waasi wa kundi la M-23.

Pamoja na kwamba Rwanda imekuwa ikipinga madai hayo, kitendo chake cha wiki iliyopita cha kuamua kupeleka bataliani mbili zenye wanajeshi 1,700 ili kukabiliana na kile kinachodaiwa kuwa ni kishindo cha vikosi vya Umoja wa Mataifa vyenye jukumu la kulinda amani katika taifa hilo lenye utajiri mkubwa kirasilimali, kinatokana na waasi wa M23 kupata kipigo kikali.

Chanzo chetu hicho kutoka uwanja wa mapambano nchini Kongo, kililidokeza gazeti hili kuwa maofisa hao wa Jeshi la Rwanda waliwakamata katika mapigano hayo yaliyodumu kwa zaidi ya wiki moja, ambayo tayari yamewakimbiza waasi wa M23.

“Askari wa Rwanda tuliowakamata, ni maofisa wa ngazi za juu kabisa jeshini, tena walikuwa na sare za jeshi hilo… walikuwa wakiwasaidia hao M23, lakini kwa kuwa sisi tulikuwa makini tulifanikiwa kuwatandika hadi tukawakamata,” kilisema chanzo chetu hicho.

Habari za uhakika kutoka vyanzo vya habari vya kuaminika zinaeleza kwamba, hatua hiyo ya kuwakamata maofisa hao pamoja na kuondoka kwa waasi wa kikundi cha M23, imefanikisha kushinda vita hiyo kwa zaidi ya asilimia 95.

Mtoa taarifa wetu huyo kutoka Kongo, ameliambia gazeti hili kuwa, tayari Monusco wanaoongozwa na JWTZ wameanza kufurahia ushindi huo na kwamba sasa hivi wanasubiri tamko kutoka kwa wakuu wao, ili kufahamu kinachofuata baada ya kufanikisha hatua hiyo.

No comments:

Post a Comment

POSTED TITLE

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...