Friday, July 12, 2013

"KILA MTANZANIA NI LAZIMA ALIPIE SH. 1000 KWA AJILI YA KADI YA SIMU YAKE"....WAZIRI WA FEDHA AMESISITIZA TENA



SERIKALI imesisitiza kuwa itatoza Sh 1,000 kwa kila kadi ya simu inayotumika lakini pia inaangalia utaratibu wa kufanya makato hayo kwa njia ambayo haitamuumiza mtumiaji wa simu.

Akizungumza jana jijini Dar es salaam, Waziri wa Fedha,Dk William Mgimwa alisema kuwa kupitia tozo hizo wanatarajia kukusanya Sh bilioni 160 kwa mwaka.
“Kupitia wawakilishi wenu na sisi serikali kuwa sikivu, tulishauriwa na ikaonekana kwamba kuna uwezekano wa kupata chanzo kingine cha mapato kupitia kadi za simu” alisema.

Alisema katika mapendekezo yaliyokuwa yametolewa serikali ilishauriwa kutoza Sh 1,450 katika kila kadi ya simu lakini baada ya kukaa na kushauriana serikali iliona ni vyema ikatoza Sh 1,000 ili kila mwananchi aweze kumudu gharama ambapo kwa mwaka kila mmiliki wa kadi ya simu atatozwa sh 12,000.
Alisema baadae serikali ilipokea mapendekezo mbalimbali ili kuangalia kama hilo linaweza kutekelezeka na walipita ngazi zote kabla halijapelekwa katika kamati za Bunge na kushauriwa kwamba tozo hilo linaweza kufanyika kwa lengo la kukuza uchumi hasa maeneo ya vijijini.
“Tathmini zote zimefanyika kikamilifu na baadae suala hilo likafikishwa Bungeni ambapo pia napo lilikubalika... inawezekana watu wanalalamika lakini ngazi zote suala hilo lilipopita lilikubalika na ikaonekana ni sawa kutozwa sh 1,000 kwa kila kadi ya simu” alisema.
Alisema kutokana na hilo kwa kutwa nzima kadi ya simu itatozwa Sh 33.35 au Sh 100 kwa siku tatu ambapo serikali inaangalia utaratibu mzuri ambao hautamuumiza mtumiaji wa simu.
Dk Mgimwa alisema fedha hizo zitakazokusanywa zitaongeza upatikanaji wa maji vijijini, umeme pamoja na kuboresha miundombinu katika maeneo ya vijijini.

No comments:

Post a Comment

POSTED TITLE

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...