Tuesday, February 9, 2016

DIAMOND AINEEMESHA UPYA FAMILIA YAKE!


DIAMOND AKIWA KWENYE PICHA YA PAMOJA NA MALIKIA WAKE TIFFAH NA MAMA TIFFAH ZARI THE BOSS LADY.

FAMILIA ya mkali wa Muziki wa Kizazi Kipya Bongo, Nasibu Abdul ‘Diamond Platinumz’ imelamba mamilioni ya shilingi kufuatia mkataba walioingia hivi majuzi na kampuni ya simu ya mkononi ya Vodacom, Risasi Mchanganyiko lina ripoti kamili.

Kwa mujibu wa chanzo kilicho ndani ya kampuni hiyo yenye mtandao mkubwa zaidi wa simu nchini, Diamond na familia yake inayowahusisha mama yake mzazi, mzazi mwenzake Zarinah Hassan na mtoto wao Tiffah, wamepewa kiasi cha shilingi milioni 700.“Mimi nipo hapa, mkataba umefanywa kwa usiri mkubwa na unajua haya mambo yanakuwaga kisheria zaidi, lakini dogo (Diamond) kalamba siyo chini ya milioni 700, nadhani ndiyo msanii wa kwanza Bongo kupata mkwanja wa maana kwenye haya matangazo ya biashara,” kilisema chanzo hicho.

Wakati chanzo hicho kikitoa madai hayo, katika baadhi ya mitandao ya kijamii, kiasi cha fedha kinachotajwa kutolewa katika mkataba huo ni kiasi cha dola 650,000.
Gazeti hili lilimtafuta Meneja Uhusiano wa Vodacom Tanzania, Matina Nkurlu ili azungumzie madai hayo ikiwemo kiasi halisi ambacho Diamond alipewa.

“Ni kweli kuwa ni jambo jema kama wasanii wachanga na wengine wakijua kiasi halisi cha fedha ambacho Diamond amepewa, ila suala hili lipo kisheria, nitakuwa nimevunja sheria endapo nitasema, kifupi ni kwamba amesaini mkataba mnono na kama Vodacom, tutaendelea kuwasapoti wasanii wetu wa ndani na maisha yao yataendelea kuwa murua.
“Tunachoomba ni kwa wasanii wetu kujituma zaidi na kuwa kioo cha jamii kwa kuwawakilisha Watanzania kwa uweledi,” alisema.

Alisema Vodacom imeingia mkataba wa mwaka mmoja na Diamond, lakini milango ipo wazi kwake kuweza kusaini upya baada ya huu kumalizika. Aidha, alisema msanii huyo ndiye pekee aliyesainishwa na kampuni yao, lakini Aprili mwaka huu, ambao ni mwezi wa kuanza kwa bajeti yao mpya, wanategemea kuwasainisha wasanii zaidi wa Bongo Fleva.

Kwa upande wake, mmoja wa mameneja wa Diamond, Babu Tale, alikiri msanii wake kupata mkataba mnono kuliko aliowahi kupata msanii yeyote kabla, lakini hata hivyo hana mamlaka ya kutaja kiasi, kwani ni suala binafsi la Diamond.

“Kwanza nikusaidie, hakuna kampuni ya ndani hivi sasa inayoruhusiwa kutoa malipo kwa dola, fedha zote zinatolewa kwa shilingi, lakini kwamba ni kiasi gani kwa kweli siwezi kusema, ila mkataba wake ni mnono kuliko msanii yeyote Bongo kwa sasa.”

Juhudi za kumtafuta mkali huyo anayetamba barani Afrika kwa sasa zilishindikana kwani hadi gazeti hili linakwenda mitamboni, taarifa zilisema alikuwa Afrika Kusini
Mtoto wa Diamond, Latiffah Nasbu ‘Tiffah’

No comments:

Post a Comment

POSTED TITLE

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...