Saturday, April 11, 2015

DIAMOND: BORA NIFE KULIKO KUMRUDIA WEMA

Musa mateja
KIAPO! Kuonesha kwamba hana mpango wa kurudi nyuma, staa wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond Platinumz’ amefungukia msimamo wake juu ya mwandani wake wa zamani, Wema Sepetu ‘Madam’ kwa kusema kuwa kamwe hawezi kumrudia tena, Risasi Jumamosi lina mkanda kamili.
Staa wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond Platinumz’.
Licha ya Diamond kufunguka hayo, wawili hao wamekuwa na mapenzi ya vipindi, kuna wakati waliwahi kumwagana kisha kurudiana na hakuna aliyewahi kutoa tamko zito lakini safari hii Diamond amesema ndiyo basi tena!
TUJIUNGE NA CHANZO
Kwa mujibu wa chanzo makini kilicho karibu na staa huyo, mara kwa mara Diamond amekuwa akijiwekea nadhiri ndani ya moyo wake na kusisitiza kwamba pamoja na kuwa maisha ya sasa huendeshwa kwa msingi wa fedha lakini hata kama ‘atafulia’ kiasi gani, ni bora afe maskini kuliko kurudiana na Wema.
“Diamond amekuwa akisema kila wakati kwa msisitizo kuwa kutokana na matatizo aliyokumbana nayo katika uhusiano wake kwa Wema, ni vigumu sana kurudiana naye wala kuwaza kama ipo siku anaweza kuwa naye, maana hakuna tena jambo geni asilolijua kwake,” kilisema chanzo hicho na kufunguka zaidi:
“Kama hiyo haitoshi, Diamond anasema anaposema haoni kitu kipya  kwa Wema anamaanisha ndiyo maana utaona leo hakuna hata siku moja ambayo amewahi kuwaza kurudiana naye hata kama atatumia ushawishi wa fedha kwa kumpelekea makontena ya fedha, hawezi kukubali anasema bora afe maskini kuliko kushea kitanda kimoja na Wema.”
DIAMOND ATHIBITISHA
Baada ya madai hayo, Risasi Jumamosi lilifanya jitihada za kukutana na Diamond uso kwa uso ambaye alithibitisha taarifa ambazo zilielezwa na mtu wake wa karibu:
“Umeambiwa na nani hayo? Sipendi kuongelea sana hivi vitu lakini huo uliousikia ndiyo ukweli. Kwa sasa nawaza maisha yangu na mpenzi wangu Zari baada ya kupitia majaribu mengi kimapenzi enzi hizo.
“Huenda wengi wasiamini ninayosema lakini nafsi yangu haijawahi kuniongoza kukumbuka ya nyuma tena kama ilivyowahi kutokea awali.
“Wengi wamekuwa wakiniuliza swali kama hili lakini sikupenda kujibu kwa kuwa nilihisi litaleta tafrani kwa mashabiki wangu, sioni sababu ya kuendelea kuulizwa kwenye media hivyo ukweli ni kwamba siwezi kurudi nyuma tena,” alisema Diamond.
Wema Sepetu ‘Madam’.
ASISITIZA KWA KUREKODI WIMBO
Kuonesha kweli amedhamiria kutogeuka nyuma, Diamond alisema kwa sasa yuko bize studio kurekodi wimbo na Nay wa Mitego (Emmanuel Elibariki) ambao utakuwa umesheheni majibu ya maswali yote ya kila kitu ambacho kilimkera kwenye uhusiano wake na Wema.“Naomba mashabiki wangu wawe na subira kwa maswali hayo yote, majibu yake yatapatikana katika project yangu na Nay inayokuja muda si mrefu,” alisema Diamond.
WEMA AJIBU MASHAMBULIZI
Alipotafutwa Wema kuhusiana na kauli hiyo ya Diamond, naye alijibu mashambulizi kwa kusema kamwe hawezi kurudiana na Diamond, hamfai hata kidogo na hata akimshawishi na  fedha nyingi kiasi gani hawezi kurudi nyuma.
“Hata aje na Bill Gates (tajiri mkubwa duniani), aje na matajiri wote anaowajua yeye duniani kamwe siwezi kulamba matapishi, kwanza sitaki kukumbuka kabisa kuhusu huyo mtu, please naomba nisimuongelee kabisa huyo mtu,” alibwatuka Wema.
WAMEFIKAJE HAPA?
Wawili hao ambao walidumu kwenye uhusiano na kupamba vyombo mbalimbali vya habari, kila mmoja amekuwa akimtuhumu mwenzake kuwa msaliti lakini sababu kubwa ambayo Diamond amekuwa akiisimamia juu ya kummwaga Wema ni baada ya mrembo huyo kuhongwa gari na mwanaume mwingine.

No comments:

Post a Comment

POSTED TITLE

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...